Mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi (TSNP), Abdul Nondo amemuomba wakili wake, Hakimu John Mpitanjia kujitoa kusikiliza na kutetea kesi inayomkabili kutokana na mambo matatu ambayo yamemfanya akose imani na Hakimu huyo.

Nondo ametaja sababu tatu za kumtaka hakimu huyo kujitoa kusimamia kesi inayomkabili sababu ya kwanza ikiwa ni madai ya Hakimu huyo kukutana na mmoja wa mashahidi na kuwahoji kama wanaendelea kuwasiliana na Nondo, ya pili Nondo amedai katika kila kesi yake inapopelekwa Mahakamani RCO wa Iringa  amekuwa akionekana kukutana na Hakimu Mpitanjia kabla na baada ya kesi hiyo.

Huku sababu ya tatu ya mshitakiwa huyo kumkataa Hakimu Mpitanjia ametaja kuwa ni mahusiano na mawasiliano mazuri na upande wa Jamhuri akiwa hana mahusiano mazuri na upande wa mshitakiwa.

Kufuatia barua iliyoandikwa na Nondo kwa Mahakama Hakimu Mkazi wa Iringa kwa madai hayo imepelekea mahakama hiyo kushindwa kusikiliza ushahidi wa mashaidi wawili kati ya watano wa kesi inayomkabili Nondo.

Abdul Nondo anashitakiwa kwa makosa mawili ambapo kosa la kwanza ni kuchapisha taarifa za uongo mtandaoni kuwa yupo hatarini akiwa katika eneo la Ubungo na kuzisambaza kwenye mtandao wa Whatsapp na kosa la pili limetajwa kuwa ni kutoa taarifa za uongo kwa mtumishi wa umma Mafinga wakati alipokuwa akitoa taarifa katika kituo cha polisi mjini humo kwa kusema kuwa alitekwa na watu wasiojulikana.

Sheria yawabana wanandoa Kenya, Hakuna kugawana 50/50
Wilfried Zaha: Siendi popote