Karibu kila kona ya dunia imewakilishwa na watu kadhaa waliotua nchini Urusi kushuhudia fainali za kombe la dunia zinazoendelea, lakini nywele za kiafrika zimegeuka ‘kitu’ kwenye saluni za wenyeji.

Raia wa Afrika Mashariki wameshuhudia hali ya tofauti inayoendelea kwenye saluni za kiume jijini Moscow, ambapo vinyozi wake ni wanawake warembo, hali inayowasababisha kufanya utafiti wa kina kabla ya kuingia saluni.

Kwa mujibu wa mwandishi wa habari, Jacob Icia ambaye anaandikia Citizen ya Kenya, aliambiwa na rafiki yake wa karibu aishie nchini humo kuwa nywele za kiafrika huwafanya vinyozi hao wanawake kuitana kujionea tofauti bila mhusika kuelewa kinachoendelea.

“Kazi ya ukinyozi hapa hufanywa zaidi na wanawake. Ni kama kazi ya wanawake. Lakini utajikuta unakuwa mfano kwani watapenda kuzichambua na kushangaa nywele zako za Kiafrika. Hautaelewa wanachokiongea lakini wasichana hao watakuwa wanawaita wenzao ili nao waziguse nywele zako,” aliambiwa na rafiki yake aliyeishi nchini humo miaka sita.

“Wanaweza hata kujidai kuwa wanakupaka kitu fulani kwa ajili ya kukunyoa ilimradi tu na wao washike nywele zako,” alielezwa.

Hali hiyo ilimlazimu Jacob kutafutiwa kinyozi mmoja maarufu ambaye ni raia wa Kenya, ambaye ameishi nchini humo akifanya kazi ya kuwanyoa watu wengi wenye asili ya Afrika Mashariki ambao wanakwepa kuingia kwenye saluni za wenyeji.

Anasema kuwa alipokuwa anayolewa na kinyozi huyo aliyedai kuwa amefanya sana kazi hiyo jijini Nairobi kabla ya kwenda Urusi, alimwambia kuwa anapata wateja wengi wenye nywele za asili ya Afrika kutokana na ukwepaji wa kuingia kwenye saluni za raia wa Urusi.

Video: Majaliwa apiga marufuku gari za serikali kulala nyumbani kwa mtu
Ajali ya Noah yaua watano Mtwara