Rais wa zamani wa Marekani, Barack Obama amewataka Wamarekani kukataa lugha za chuki na kibaguzi kutoka kwa viongozi wao.

Ametoa kauli hiyo wakati rais wa nchi hiyo, Donald Trump akiwa katika harakati za kujinasua kwa kauli zake dhidi ya wahamiaji ambazo ndiyo zinasemekana kuwa chanzo cha kuchochea mauaji nchini humo.

Akiwa madarakani, Obama alipigania suala zima la umiliki wa silaha za moto kuwa na utaratibu maalum lakini hakuweza kufanikiwa.

Katika mahojiano yake na shirika la utangazaji la BBC yaliyofanyika mwaka 2015,  Obama alisema kuwa kushindwa kupitishwa kwa sheria za kudhibiti silaha ndilo jambo kubwa alilofeli akiwa kama kiongozi wa nchi hiyo.

Mwishoni mwa wiki iliyopita jumla ya watu 31 waliuawa katika mashambulio ya bunduki kwenye majimbo ya Texas na Ohio.

Aidha, Obama amekuwa akikwepa kuzungumzia sera za Trump, hususani ya uhamiaji ambayo imekuwa ikipingwa na makundi tofaouti, hata hivyo, safari hii ametoa tamko.

“Inabidi kwa pamoja tukatae lugha zinazotoka kwenye kinywa cha kiongozi wetu yoyote ambaye analisha mazingira ya uoga na chuki ama anayefanya ubaguzi kuwa jambo la kawaida. Viongozi ambao wanawafanya watu ambao hawafanani nasi kuonekana kama mashetani, ama wanaodai kuwa watu wengine ikiwemo wahamiaji wanahatarisha mfumo wetu wa maisha, ama wanaodai kuwa Marekani ni ya jamii moja tu ya watu,” amesema Obama

Madaktari waelezea 'mtihani' baada ya mtoto wa dereva wa RC-Mara kufariki
Serikali kuhakikisha wanufaika wa TASAF wanapata ruzuku kwa wakati