Klabu ya Olympic Marseille imeonyesha nia ya kukutana na uongozi wa Chelsea, kwa ajili ya kufanya biashara ya usajili wa mshambuliaji kutoka nchini Ufaransa Olivier Giroud.

Gazeti la Mirror Football limetoa taarifa zinazoeleza kuwa, klabu hizo mbili huenda zikaanza kufanya mazungumzo wakati wowote juma hili, baada ya Chelsea kudhihirisha mpango wa kumuweka sokoni Giroud.

Mbali na Giroud, klabu ya Olympic Marseille pia inatajwa kuwa katika hatua za kumsajili mshambuliaji Super Mario Balotelli kutoka Nice, na inaaminika wawili hao wakitengeneza ushirikiano mzuri kwenye kikosi cha klabu hiyo, mambo yatawaendelea vyema msimu wa 2018/19 ambao utaanza rasmi mapema mwezi ujao.

Giroud, mwenye umri wa miaka 31, anatarajia kuondoka Chelsea baada ya kuitumikia klabu hiyo kwa miezi mitano, akitokea Arsenal ambayo ilimuuza dakika za lala salama wakati wa usajili wa dirisha dogo mwezi Januari.

Harakati za kuuzwa kwa Giroud, zinatoa nafasi kwa Chelsea kutimiza lengo la kukamilisha hatua za kumsajili mshambuliaji kutoka nchini Argentina na mabingwa wa soka Italia Juventus FC, Gonzalo Higuain.

Meneja mpya wa klabu ya Chelsea Maurizio Sarri amekua mstari wa mbele katika kuhakikisha usajili wa mshambuliaji huyo unafanikiwa kabla ya kufungwa kwa dirisha la usajili wa majira ya kiangazi mapema mwezi ujao.

Lowassa kutoa baraka kwa Freddy kugombea Monduli
Mfuko mpya wa Hifadhi ya Jamii PSSSF kuanza kazi Agosti Mosi