Kocha Mkuu wa Mabingwa wa Soka Tanzania Bara Pablo Franco Martin amesema kikosi chake kina wachezaji wenye sifa ya kupambana wakati wote, hali ambayo anaamini itaweza kumtimizia malengo yake msimu huu 2021/22.

Kocha Pablo ametoa sifa hizo baada ya kukishuhudia kikosi cha Simba kikicheza mchezo wa Ligi Kuu dhidi ya Ruvu Shooting kisha mchezo wa Kirafiki dhidi ya Green Warriors.

Simba SC iliifunga Ruvu Shooting mabao 3-1 siku ya Ijumaa (Novemba 19) Uwanja wa CCM Kirumba Jijini Mwanza, maboa yakifungwa na Meddie Kagere aliyefunga mawili na Kibu Denis.

Katika mchezo wa Kirafiki dhidi ya Green Warriors uliopigwa Uwanja wa Mo Simba Arena Jumapili (Novemba 21), Simba SC iliibuka na ushindi wa mabao 4-0.

Kocha huyo kutoka nchini Hispania amesema wachezaji wake wana uwezo mzuri na mkubwa kisoka, hivyo anachopaswa kukifanya ni kuwaunganisha lakini pia kuwajengea kujiamini zaidi.

Pablo pia ameeleza furaha yake kwa kurejea kwa wachezaji ambao walikuwa majeruhi, huku akiweka wazi kama watakuwa fiti kwa asilimia 100, ana uhakika watafanya vizuri katika mchezo ujao wa Kombe la Shirikisho Barani Afrika ‘CAF’ dhidi ya Red Arrows na michezo ya Ligi Kuu dhidi ya Geita Gold na Young Africans.

“Nimewaona wachezaji karibu wote, naendelea kuwasoma na kutafuta muunganiko mzuri, ili kuweza kukabiliana na michezo iliyopo mbele yetu na hata dhidi ya Yanga,” amesema Kocha Pablo.

Simba SC itacheza mchezo wa Hatua ya Mtoano Kombe la Shirikisho Barani Afrika mkondo wa kwanza Jumapili (Novemba 28) dhidi ya Red Arrows kutoka Zambia, Uwanja wa Benjamin makapa.

Mchezo wa Mkondo wapili utachezwa Desemba 5, nchini Zambia.

Mangungu: Tutatoboa Jumapili
Maji Dar bado hali si shwari - Aweso