Bondia Mfilipino, Manny Pacquiao leo amepata mpinzani mpya ambaye anapewa nafasi zaidi ya kupanda naye ulingoni hivi karibuni, baada ya Floyd Mayweather kuendelea kuwa kimya kuhusu uwepo wa  pambano la marudiano.

Pacquiao ambaye leo alikuwa kwenye mzungoko wa ulingo akishuhudia pambano kali kati ya bondia Errol Spence Jr. na Mikey Garcia, ameshuhudia Spence Jr. akimchakaza vikali mpinzani wake huyo, akishinda karibu raundi zote.

Hata hivyo, Mikey Garcia ambaye amepoteza kwa mara ya kwanza ulingoni (7-1), amesifiwa kwa jinsi alivyoweza kustahimili pambano hilo lililomalizika leo asubuhi kwa saa za Afrika Mashariki, kwani alilazimika kupanda uzito ili akabiliane na Spence Jr. ambaye amekuwa na rekodi nzuri akiwa hajapoteza mapambano yake 25 sasa.

Spence Jr. alishusha makonde 345 dhidi ya 75 ya mpinzani wake huyo kwa mujibu wa program ya kurekodi matukio ya masumbwi, na kufanikiwa kuendelea kuwa bingwa wa masumbwi wa dunia uzito wa welterweight wa IBF.

Manny Pacquiao anatarajia kupanda ulingoni Julai mwaka huu na kwa sasa Spence Jr. ndiye anayetarajiwa kupanda naye ulingoni katika pambano ambalo linatarajiwa kuitwa pambano la mwaka katika uzito huo.

“Je, hili ndilo pambano unalolitaka Manny,” mtangazaji alimuuliza, “ndio, kwanini lisiwe… tutawapa mashabiki kitu wanachokitaka,” alijibu bondia huyo ambaye pia ni Seneta nchini kwake.

Spence Jr. ni kati ya mabondia wawili ambao wamekuwa wakitajwa kuwa wana uwezo wa kumstaafisha Pacquiao.

Majaliwa awatahadharisha wadau wa madini, 'Hatua kali za kisheria zitachukuliwa'
Wazazi wa wanafunzi wanaodai kulishwa vyakula vilivyooza wavamia shule