Manchester City wametwazwa kuwa mabingwa wa ligi ya England msimu wa 2017/18 kupitia mgogo wa mahasimu wao Manchester United, kufuatia matokeo ya mchezo wao wa jana dhidi ya West Brom

Manchester United walikubali kufungwa bao moja kwa sifuri wakiwa nyumbani Old Traffford dhidi ya West Brom, ambao wanaendelea kuhangaika kujiondoa katika mkia wa msimamo wa ligi ya England.

Kupoteza mchezo huo, kumeifanya Manchester United kuwa nyuma kwa alama 16 dhidi ya mahasimu wao Manchester City, huku michezo mitano ikisalia kwa kila mmoja.

Kimahesabu Manchester United hawatoweza kuzifikia alama za 87 zinazomilikiwa na Manchester City, hata ikitokea wanashinda michezo yao iliyosalia.

Mpaka sasa, Manchester United wamejikusanyia alama 71 na wapo katika nafasi ya pili kwenye msimamo wa ligi.

Kwa mantiki hiyo Manchester City wamefikia lengo la kutwaa ubingwa wa ligi ya England msimu huu, na kufikkisha taji la tatu tangu walipoanza kuwa chini ya tajiri wa kiarabu Sheikh Mansour bin Zayed Al Nahyan .

Pia taji la ligi la msimu huu, linakua la kwanza kwa meneja kutoka nchini Hispania Pep Guardiola ambaye aliajiriwa klabuni hapo mwaka 2016 akitokea FC Bayern Munich, Ujerumani.

Guardiola kwa msimu huu ameiwezesha Manchester City kutwaa mataji mawili likiwepo taji la Carabao (Kombe La Ligi) walilolichukua baada ya kuifunga Arsenal katika mchezo wa fainali mwishoni mwa mwezi Februari.

Kwa mantiki hiyo, Guardiola anafikisha mataji 24 tangu alipoanza shughuli za ukufunzi wa soka akiwa na klabu ya FC Barcelona aliyoitumikia kuanzi mwaka 2008–2012 na baadae Bayern Munich mwaka 2013–2016.

Wakati huo huo Manchester City wanafikisha taji la saba tangu walipoanza kuwa chini ya umiliki wa Sheikh Mansour bin Zayed Al Nahyan mwaka 2008. Miongoni mwa mataji hao ni kombe la FA mara mbili, kombe la ligi mara mbili, Ngao ya Jamii mara tatu.

Aliyedai kutelekezwa na Lowassa aomba radhi
AS Monaco yawaomba radhi mashabiki, kurudisha fedha za viingilio