Meneja wa klabu bingwa nchini England (Manchester City), Pep Guardiola amefungiwa na shirikisho la soka barani Ulaya (UEFA), kukaa kwenye benchi la klabu hiyo kwa michezo miwili, baada ya kukutwa na hatia ya utovu wa nidhamu.

Guardiola ameadhibiwa kutokana na kitendo cha kumtoea maneno makali mwamuzi aliyechezesha mchezo wa robo fainali wa ligi ya mabingwa dhidi ya Liverpool ambao ulichezea April 10 kwenye uwanja wa Etihad.

Meneja huyo mwenye umri wa miaka 47, aliamuriwa kukaa jukwaani baada ya kuonyesha utovu wa nidhamu dhidi ya mwamuzi, na baadae UEFA walimfungulia mashataka.

Hata hivyo meneja huyo wa zamani wa FC Barcelona alipata nafasi ya kujitetea kabla ya maamuzi ya kufungiwa hayajatangazwa dhidi yake, na kikubwa alichosema “Sikumtukana mwamuzi Mateu Lahoz, nilimwambia wazi kuhusu kulikataa bao letu lililofungwa na Sane dakika chache kabla ya kipindi cha kwanza hakijamalizika.”

Kwa upande wa Majogoo wa jiji Liverpool, nao wametozwa faini na shirikisho hilo ya euro 30,000 sawa na Pauni 25,450, kufuatia vurugu zilizoonyeshwa na mashabiki wao, wakati wa michezo ya robo na nusu fainali.

Liverpool pia wamekumbana na faini nyingine ya Euro 20,000 sawa na Pauni 17,500, baada ya kubainika mashabiki wa klabu hiyo walilirushia mawe basi la wachezaji wa Man City wakati lilipokua likiwasili kwenye uwanja wa Anfield Aprili 04.

Faini nyingine kwa Liverpool ni Euro 6,000 sawa na Pauni 5,200 ambayo imesababishwa na vitendo vya mashabiki wao kuwasha miale ya moto na kuirusha sehemu ya kuchezea wakati wa mchezo wa mkondo wa pili dhidi ya Man City, na faini nyingine ni Euro 3,000 sawa na Pauni 2,600 ambayo imetokana na kitendo kama hicho, wakati wa mchezo wa mkondo wa pili wa nusu fainali dhidi ya AS Roma.

Jafo awataka waamuzi UMISSETA na UMITASHUMTA kuzingatia kanuni
Jordan Pickford akabidhiwa gwanda England