Hatimaye aliyekuwa Katibu Mkuu wa Chama Cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Wilbroad Slaa amekamilisha ndoto yake kubwa baada ya jana kufunga ndoa na mpenzi wake, Josephine Mushumbusi nchini Canada.
Ingawa Dk. Slaa aliwahi kuwa Padri wa Kanisa Katoliki, wawili hao wanadaiwa kufunga ndoa kwenye kanisa tofauti la Kikristo ingawa jina la kanisa hilo halikufahamika mara moja.
Jaribio la kufunga ndoa kwa wawili hao tangu mwaka 2010 lilikumbwa na vizingiti ikiwa ni pamoja na mume wa zamani wa Josephine kufungua kesi mahakamani akidai kuwa bado mwanamke huyo ni mkewe halali.
Kadhalika, Mke wa Dk. Slaa, Rose alifungua kesi mahakamani mwaka 2012 akipinga wawili hao kufunga ndoa akidai malipo ya shilingi milioni 50. Hata hivyo, madai yote hayo yamebaki kuwa historia baada ya tukio hilo la jana.
Dk. Slaa alitangaza kustaafu Siasa mwaka jana na kuelekea nchini Canada ambapo anajiendeleza kimasomo na kutumia muda huo kuwa na mkewe Josephine.