Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi, Humprey Polepole amempongeza Waziri Mkuu wa Zamani, Edward Lowassa kwa uamuzi wake wa kurejea kwenye chama hicho baada ya takribani miaka minne.

Lowassa aliachana na CCM Julai 2015 katika harakati za Uchaguzi Mkuu, baada ya kutoridhishwa na uamuzi wa Kamati Kuu kulikata jina lake kwenye kinyang’anyiro cha wagombea urais na alijiunga na Chadema ambapo alipewa nafasi hiyo. Hivi karibuni, alitangaza kurejea tena CCM.

Jana, Lowassa alipokelewa kwa kishindo nyumbani kwake Monduli, kwa mara ya kwanza baada ya kuchukua uamuzi wa kurejea ndani ya chama hicho anapokuita ‘nyumbani’.

Polepole aliyekuwa miongoni mwa viongozi waandamizi wa CCM waliompokea Lowassa Monduli, aliuelezea uamuzi huo kama ukomavu wa kisiasa.

“Leo kwa roho njema ya kupatana tunapata kusimama pamoja, tuchape kazi tupeleke mbele taifa letu la Tanzania,” alisema Polepole.

Alisema kuwa anampongeza Lowassa kwakuwa amekomaa kisiasa kwa kuweka maslahi ya Taifa mbele. Taifa linataka mshikamano, taifa linataka umoja na kusonga mbele.

Rosa Ree kupata mtoto, kukamilisha safari ya kuwa mama
Vanessa awatolea uvivu waliodai hakumzika Ruge, Kibonde