Kitendo cha askari polisi kumpigia saluti Mwenyekiti wa Chama Cha Wananchi (CUF) anayetambuliwa na Ofisi ya Msajili wa vyama vya siasa, Profesa Ibrahim Lipumba imezua gumzo la kuhoji uhalali wake.

Askari huyo alionekana juzi akimpigia saluti Profesa Lipumba katika eneo la Buguruni ambapo mwanasiasa huyo alienda kushiriki zoezi la usafi.

Kamanda wa Polisi mkoa wa Ilala, Salum Hamduni alipoulizwa kuhusu usahihi wa askari polisi kuwapigia saluti viongozi wa vyama vya siasa wasio wabunge alijibu kwa ufupi, “sio sawa.”

Kwa mujibu wa Kanuni za Jeshi la Polisi (PGO) namba 102, haiwataji viongozi wa vyama vya siasa wasio wabunge kati ya watu wanaopaswa kupewa salamu hiyo ya jeshi yenye kuonesha heshima.

Aliyekuwa Naibu Waziri wa Mambo ya Ndani wa Serikali ya Awamu ya Tatu, Kapteni John Chiligati aliwahi kueleza Bungeni kuwa saluti ni ishara ya kuonesha heshima kwa kiongozi mkuu kwenye asasi za kijeshi.

Kapteni Chiligati alisema kuwa mbali na viongozi wa kijeshi, viongozi wengine wanaopaswa kupewa saluti ni wa mihimili ya Serikali, Bunge na Mahakama.

Wengine ni majaji wote, wabunge, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya na mahakimu wa mikoa na wilaya wakiwa kwenye mahakama zao.

Katibu Mkuu wa Chama Cha CCK, Renatus Muabhi alisema kuwa huenda askari huyo alipiga saluti kwa kupaniki kutokana na maagizo aliyopewa ya kumlinda Profesa Lipumba katika zoezi hilo.

Mmoja afariki baada ya basi, Lori kuteketea kwa moto
Lowassa, Sumaye waweka mkakati mzito na wabunge wa Ukawa Dodoma