Jeshi la Polisi Kanda Maalum ya Dar es Salaam limesema kuwa Dk. Louis Shika ambaye alishinda mnada wa ununuzi wa nyumba za Said Lugumi na baadae kuzua kizaa-zaa, alitumwa na Lugumi mwenyewe.

Dk. Louis ambaye alifunga mnada wa nyumba hizo kwa kuahidi kulipia shilingi milioni 900, alishindwa hata kutoa robo ya kiasi hicho kwa mujibu wa masharti ya mnada hali iliyopelekea kufikishwa katika kituo cha polisi.

Kamanda wa Jeshi la Polisi wa kanda hiyo, Lazaro Mambosasa amesema kuwa jeshi hilo linahisi kuwa alitumwa na Lugumi kutokana na mazingira ya tukio husika.

“Aliwekwa na Lugumi ili kukwamisha mnada,” Mambosasa anakaririwa na Mwananchi ingawa aliweka angalizo kuwa hana vielelezo kuhusu hilo.

“Ingawa sina facts (vielelezo) kuthibitisha hilo, lakini alichokuwa anafanya kinatufanya tuamini hivyo. Kwasababu alikuwa anapandisha bei kila nyumba ili washiriki wengine wasinunue,” aliongeza.

Alisema kuwa hata muonekano wa mnunuzi huyo ulikuwa unatia shaka na kwamba Jeshi hilo linaendelea kumshikilia kwa mahojiano zaidi.

Dkt. Willbroad Slaa ageuka mhudumu Canada
Majaliwa apangua hoja ya Katiba Mpya