Jeshi la Polisi linamsaka mtu mmoja anaetumia akaunti ya Twitter kwa jina la aliyekuwa Gavana wa Benki Kuu, Daudi Balali.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Habari na Mahusiano wa Jeshi la Polisi nchini, Bi. Advera Bulimba, jana aliwaambia waandishi wa habari kuwa tayari jeshi hilo limebaini uwepo wa akaunti hiyo na wanafanya uchunguzi wa kina ili kumtia mbaloni mhusika huyo.
“Tuna taarifa juu ya ukurasa huo wenye wafuasi wengi kwa sasa na unatumika kuwashambulia viongozi wa serikali na wanasiasa hususan wale wanaogombea nafasi kubwa za utawala nchini,” alisema. “Jeshi la polisi liko kwenye uchunguzi ili kumbaini mtu huyo haraka iwezekanavyo,” aliongeza.
Aliwaonya watu wanaofanya uhalifu kupitia mitandao kuwa watakumbana na mkono wa dola kwa kuwa jeshi hilo lina njia nyingi za kuwabaini watu hao kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA).
John – unafahamu wamiliki wa hivyo viwanda wengi wako ndani ya CCM? Toa mkakati wa kusafisha CCM kabla ya Ilani. https://t.co/M0WAqz6mZD
— Balali, DTS (@daudibalali) September 9, 2015
Ukurasa huo wenye wafuasi zaidi ya 7200, hutumika kuwashambulia viongozi wa serikali na wanasiasa mbalimbali huku mtu huyo akisisitiza kuwa yeye ni ‘Balali’ halisi na kwamba watu wasiamini kama alifariki huku akiahidi kuwa ipo siku atajitokeza hadharani.