Mwanamke mwenye umri wa miaka 41 ameuawa huku mwanaume aliyekuwa naye mwenye umri wa miaka 26 akijeruhiwa vibaya kwa risasi zilizofyatuliwa na polisi kuelekea kwenye gari lao jijini Nairobi nchini Kenya.

Jeshi la polisi limeeleza kuwa tukio hilo lilitokea baada ya watu waliokuwa katika eneo hilo kutoa taarifa ya kulitilia shaka gari aina ya Toyota Fielder KBX 515 H, lililokuwa limepaki kwa muda kidogo katika eneo moja la City Park, likiwa limefungwa vioo vyeusi (tinted).

Kwa mujibu wa jeshi hilo, Maafisa wake baada ya kujipanga walienda kugonga kwenye dirisha la gari hilo lakini liliondoshwa ghafla na kwa mwendo mkali kuelekea barabarani, hali iliyowalazimu kuanza kuishambulia kwa risasi ili isitokomee.

“Baada ya kusimama, ndani tulikuta mwanamke mwenye umri wa miaka 41 ambaye baadaye alitambuliwa kwa jina la Janet Wangui pamoja na mwanaume ambaye alitambulika baadaye kwa majina ya Benard Chege, wote wakiwa Wakikuyu,” imeeleza sehemu ya taarifa ya jeshi la Polisi.

Taarifa hiyo ilingeza kuwa wawili hao walikuwa nusu utupu wakiwa na majeraha ya risasi. Walikimbizwa hospitalini ambapo Chege alipata matibabu lakini Madaktari walibainisha kuwa Janet alikuwa ameshafariki.

Kutokana na mazingira hayo, imeelezwa kuwa huenda watu hao walikuwa wanajaribu kufanya mapenzi kwenye gari hilo. Upelelezi wa tukio hilo umeanza mara moja, kwa mujibu wa maafisa wa jeshi la polisi.

Magazeti ya ndani na nje ya Tanzania leo Mei 22, 2018
Video: Chama nacho tumeamua kukisafisha na mambo ya rushwa- JPM