Chama cha soka nchini England (FA) kimemfungulia mashataka meneja wa klabu ya Newcastle United Rafael Benitez, kufuatia kauli aliyoitoa dhidi ya mwamuzi Andre Marriner, kabla ya kuanza kwa mchezo wa ligi kuu dhidi ya Crystal Palace waliokua nyumbani Selhurst Park mwishoni mwa juma lililopita.

Benitez alihojiwa na kituo cha televisheni cha Sky Sports na kusema, mwamuzi huyo amekua hana historia nzuri na wachezaji wa Newcastle Utd, hivyo hakutarajiwa kama angetendewa haki.

“Mwamuzi huyu hana historia nzuri na wachezjai wangu, ameshawahi kuwapa kadi nyekundu mara kwa mara, sijui kama tutatoka salama leo ” alisema meneja huyo kutoka nchini Hispania.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na FA kupitia ukurasa wake wa Twitter, Benitez ametakiwa kuwasilisha utetezi wake kabla saa kumi na mbili jioni kwa saa za England, siku ya ijumaa.

Katika mchezo huo Newcastle Utd walilazimisha matokeo ya sare ya bila kufungana dhidi ya wenyeji wao Crystal Palace.

Vivuko vya Kigamboni kusitishwa, daraja la Nyerere kutumika
Lionel Messi, Cristiano Ronaldo wamtibua Fabio Capello