Aliyekua Mwenyekiti wa klabu ya Simba Ismail Aden Rage amelitaka shirikisho la mpira wa miguu Tanzania TFF kufuata kanuni za CAF ilii kufidia gharama walizoingia baada ya timu ya Chad kujitoa kushiriki michuano ya kufuzu kwa fainali za mataifa ya Afrika (AFCON) kutokana na ukata.

Rage alisema kuwa tayari TFF imeingia hasara kubwa baada ya Chad kujitoa dakika za majeruhi huku maandalizi ya mechi ya kimataifa yakiwa yamekamilika kwa kiasi kikubwa hivyo amelitaka shirikisho hilo kufuata kanuni za CAF ili kupata fidia ya gharama zilizotumika.

“Kwa kufuata kanuni za CAF za kujitoa mashindanoni ghafla lazima kuna asilimia unazipata kutoka kwenye chama cha soka cha nchi husika ili kufidia hasara hata kama sio asilimia mia moja.” alisema Rage.

Leo shirikisho la mpira wa miguu Tanzania TFF litarudisha pesa za kiingilio kwa washabiki waliokata tiketi kwa ajili ya kutazama mechi ya Taifa Stars dhidi ya Chad baada ya wageni kujitoa dakika za majeruhi huku gharama za kuweka timu kambini pamoja na maandalizi ya mchezo zikiwa ndiyo zimepotea.

Rais  wa TFF Jamal Malinzi alinukuliwa akisema hajawahi kufikiria kutokea kwa tukio hilo  na kutanabaisha bado hakuwa na jibu la moja kwa moja la sakata hilo.

Kwa mujibu wa ratiba ya CAF Stars ilikuwa icheze mechi ya marudiano jana March 28 dhidi ya Chad baada ya kupata ushindi wa goli 1-0 mjini N’Djamena Jumatano iliyopita.

Bausi: Nitagombania Urais Wa ZFA
Lowassa atoa ahadi kuhusu Zanzibar