Raia wa Liberia Musa Bility ameondolewa kutoka kwenye kinyang’anyiro cha kuwania urais wa Fifa kwa sababu ya maadili.

Shirikisho hilo linalosimamia soka duniani limeidhinisha wagombea watano pekee. Mkuu wa Uefa Michel Platini pia hajajumuishwa kwenye orodha hiyo ya wagombea.

Mfaransa huyo hata hivyo huenda akaongezwa iwapo marufuku yake itamalizika kabla ya uchaguzi kuandaliwa Februari.

Mwanamfalme Ali bin al-Hussein, Jerome Champagne, Gianni Infantino, Sheikh Salman bin Ebrahim al-Khalifa na Tokyo Sexwale ndio pekee walioidhinishwa.

FIFA imesema haitazungumzia zaidi sababu za kutemwa kwa Bility, ambaye anaweza kupinga uamuzi huo katika mahakama ya kutatua mizozo ya michezo. Imesema imeamua kutofichua maelezo zaidi kuhusu sababu hizo kwa maslahi ya Bility.

Bility ndiye rais wa shirikisho la soka la FA.

Uchaguzi huo utachagua mrithi wa Sepp Blatter, ambaye amesimamishwa kazi na anachunguzwa kwa tuhuma za ufisadi.

Blatter, 79, alitangaza atajiuzulu mwezi Juni baada ya Fifa kukumbwa na kashfa ya ufisadi.

Wagombea waliosalia Fifa

  • Mwanamfalme Ali bin al-Hussein, 39, ndiye rais wa Shirikisho la Soka la Jordan.
  • Jerome Champagne, 57, ni afisa mkuu mtendaji wa zamani wa Fifa.
  • Gianni Infantino, 45, ndiye katibu mkuu wa Uefa
  • Michel Platini, 60, ndiye rais wa Uefa na naibu rais wa Fifa (Ugombea wake bado haujaidhinishwa.)
  • Sheikh Salman bin Ebrahim al-Khalifa, 49, ndiye rais wa Shirikisho la Soka la bara Asia
  • Tokyo Sexwale, 62, ni waziri wa zamani wa Afrika Kusini

Marc Wilmots Amuweka Pembeni Vincent Kompany
Unyama: Msichana Asimulia Alivyobakwa Zaidi Ya Mara 43,000