Rais aliyeondolewa madarakani na Bunge nchini Peru, Pedro Castillo amewekwa chini ya kizuizi cha muda siku moja baada ya kuvuliwa wadhifa wake na bunge la nchi hiyo kwa tuhuma za kufanya uasi na kuvunja katiba.

Jana (Alhamisi ya Desemba 8, 2022), ikiwa ni siku moja baada ya kuondolewa madarakani, Castillo alikuwa chini ya kizuizi cha muda na kisha baadaye alifikishwa mbele ya Mahakama ya Juu ya nchi hiyo kwa njia ya video.

Aidha, inaarifiwa kuwa, Waendesha mashtaka, walifanya upekuzi kwenye ofisi za Rais na baadhi ya majengo ya Wizara kutafuta ushahidi dhidi ya Castillo, anayechunguzwa kwa uasi na njama dhidi ya taasisi za dola.

Mwanasiasa huyo wa mrengo wa kushoto, alipandishwa kizimbani kwa muda mfupi na waendesha mashtaka walimwomba Jaji atoe idhini kwa vyombo vya dola kuendelea kumshikilia kwa muda wa wiki moja.

Jaji anayesikiliza kesi hiyo aliridhia ombi hilo la waendesha mashtaka licha ya hoja za wakili wa Castillo aliyesema hakuna kosa la uasi lililotendwa na mwanasiasa huyo.

Hata hivyo, Castillo hakusema jambo lolote na alijibu maswali machache Mahakamani kuhusiana na mipango yake ya kulivunja bunge na kutawala kwa amri badala ya katiba.

Chanjo ya Ebola yawasili baada ya siku 42 bila kesi mpya
Vita ya Malaria: Msaada wa kifedha wahitajika