Rais wa zamani wa Shirikisho la Soka Duniani (FIFA) na Shirikisho la Soka la Brazil Joao Havelange, alifariki dunia Jana akiwa na umri wa miaka 100. Joao Havelange alikuwa akiugua maradhi ya muda mrefu yanayosemekana kuwa ni Pneumonia yanayoathiri mapafu.

Joao Havelange alikuwa Rais wa FIFA kwa takribani miongo miwili, huku pia akiongoza chama cha soka nchini kwao, Brazil. Gwiji huyu alikiongoza chama cha soka nchini Brazil katika kipindi cha miaka 1956 mpaka 1974. Pia alikuwa Rais wa FIFA kwa miaka 24 yaani 1974 mpaka 1998.

Taarifa zilizotolewa na vyombo vya habari vya Brazil zinasema kuwa Havelange alifariki asubuhi ya Jumanne kwa saa za Brazil. Andresa Feijo ambaye ni msemaji wa hospitali aliyokuwa amelazwa Havelange, alithibitisha kutokea kwa kifo cha gwiji huyu. Aliweka wazi pia kuwa amekuwa akitibiwa Pneumonia tangu mwezi Julai.

Havelange alikuwa ni moja ya watu muhimu sana waliosaidia Brazil kushinda uenyeji wa michuano ya kombe la dunia mwaka 2014 na ile Olimpiki inayoendelea huko katika zaidi ya majiji matano chini humo.

Pamoja na kuwa mtu muhimu sana kwenye historia ya soka duniani kwa maana ya kulikuza kibiashara na kufika kwake kwenye mataifa mbalimbali, Havelange alikumbwa na kashifa nyingi za rushwa ambazo ziliathiri heshima yake kwenye soka.

Mwaka 2013, Havelange alijiondoa kuwa Rais wa heshima wa shirikisho la soka duniani FIFA, baada ya kusemekana kuwa alipokea hongo/rushwa.

Havelange atakumbukwa kwa kitendo chake cha kuweza kuongeza idadi ya nchi shiriki kwenye mashindano ya kombe la dunia kutoka timu 16 mpaka 32.

Lakini pamoja na hayo alisimamia na kuandaa mashindano ya kombe la dunia mara 6 tofauti huku akiwa chanzo cha mikataba mikubwa ya kibiashara ya chama hicho na pia anakumbukwa kwa kuwa chanzo cha kutambulika kwa soka la wanawake.

UEFA Kuomba Ridhaa Ya Wajumbe, Kubadilisha Kanuni Za Ligi Ya Mabingwa
Akamatwa kwa kuwapa ombaomba maandazi yenye sumu nje ya Msikiti