Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,  Dk. John Pombe Magufuli ametangaza kumfukuza kazi mtumishi wa serikali katika Halmashauri ya Kilosa mkoani Morogoro, Daniel Elimringi, kwa kuchana kitabu kitakatifu cha Kurani kisha na kukitemea mate

Uamuzi huo ameutoa leo Februari 11, 2020 alipokuwa akizindua ofisi za wilaya ya Kigamboni jijini Dar es Salaam.

”Juzi nilikuwa namsikia mheshimiwa Jafo , mtu mmoja kule Kilosa nafikiri alichana kitabu kitakatifu, nakushukuru umechukua hatua ya kumsimamisha kazi lakini mimi ninamfukuza moja kwa moja muandikie barua ya kuondoka moja kwa moja, ashinde kesi asishinde huyo si mfanyakazi wa serikali hatuwezi kukaa na wafanyakazi wapumbavu katika serikali hii”. amesema Rais Magufuli

Juma lililopita Waziri wa nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa, Selemani Jafo aliagiza kusimamishwa kazi kwa mtumishi wa Halmashauri ya Kilosa mkoani Morogoro Daniel Elimringi, kwa kosa la kuchana kitabu cha dini ya Kiislamu, Kurani.

“Jambo hili lililofanywa na mtumishi huyu halileti kabisa afya kwa taifa letu kwani watu wake wa dini zote wamekuwa wakiishi katika mazingira ya amani na kuheshimia kwa kila mtu,” alisema Jafo.

Kauli hiyo ya Jafo, inakuja baada ya kusambaa kwa picha katika mitandao mbalimbali ya kijamii zikimuonyesha mtumishi huyo katika Halmsahauri ya Kilosa kitengo cha biashara idara ya fedha akichana na kutupa kitabu cha Kurani.

 

LIVE KENYA: Mazishi ya Rais Moi
Virusi vya Corona: Mamia ya Waganda walilia kwenda China, Serikali yawashangaa