Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Dkt. John Magufuli amemteua Rais Mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa kumuwakilisha katika maadhimisho ya miaka 50 ya mkutano wa pili wa chama tawala cha Msumbiji (FRELIMO) .

Maadhimisho hayo yatafanyika tarehe 25, Julai katika jimbo la Niassa ambapo kutokana na majukumu mengine ya kitaifa Rais amemuagiza Mkapa kumuwakilisha ambaye ataongozana na Makamu Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (Bara), Philip Mangula.

Kupitia taarifa iliyotolewa leo na Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali,Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, imesema kuwa Mkapa na mjumbe wake wanatarajia kuondoka nchini tarehe 24 Julai, 2018 na kurejea tarehe 26 Julai, 2018.

“Rais wa Jamhuri ya Msumbiji, Mhe. Filipe Nyusi alimwalika Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi (CCM), Mhe. Dkt. John Pombe Magufuli kushiriki maadhimisho hayo. Kutokana na majukumu mengine ya kitaifa Mhe. Rais Magufuli hatoweza kushiriki”, imesema taarifa.

Aidha taarifa imeongeza kuwa Tanzania na Msumbiji zimeendelea kushirikiana katika masuala ya kiuchumi na biashara kwa kuzingatia ujirani na muingiliano mkubwa wa wananchi wa nchi hizi mbili, hususani katika Mikoa ya Ruvuma na Mtwara kwa upande wa Tanzania, na Majimbo ya Niassa na Cabo Delgado kwa upande wa Msumbiji.

Video: Fahamu mnyama anayependa ngono zaidi duniani
Jose Mourinho amtumia salamu Paul Pogba