Rais wa Tanzania Dk. John Pombe Magufuli, leo 10 Oktoba, 2016 amepokea hati za utambulisho za mabalozi wanne wanaoziwakilisha nchi zao hapa nchini.

Rais Magufuli amepokea hati hizo Ikulu jijini Dar es salaam kutoka kwa Balozi wa Jamhuri ya Sudan hapa nchini, Mahjoub Ahmed Abd Allah Sharfi, Balozi wa Jamhuri ya Slovakia hapa nchini, Frantisek Dlhopolcek, Balozi wa Ukraine hapa nchini, Yevheni Tsymbaliuk na Balozi wa Jamhuri ya Ghana, Kwame Asamoah Tenkorang.

Akizungumza na Mabalozi hao kwa nyakati tofauti baada ya kupokea hati zao za utambulisho, Rais awamesisitizia umuhimu wa kuendeleza na kuimarisha uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na nchi hizo kwa kujikita zaidi katika biashara na uwekezaji.

Rais Magufuli amemwambia Balozi wa Sudani kuwa anatambuwa kuwa Sudani ina utajiri wa mafuta na imefanikiwa kujenga uchumi wake kupitia mafuta, amesema hapa nchini pia tumebaini uwepo wa mafuta na gesi asilia katika baadhi ya maeneo, hivyo angependa uhusiano na ushirikiano kati ya Tanzania na Sudani sasa ujielekeza katika kubadilishana uzoefu na ujuzi wa namna tunavyoweza kunufaika na mafuta na gesi.

Magufuli pia ametoa wito kwa wafanyabiashara na wawekezaji kutoka nchi za Sudan, Slovakia, Ukraine na Ghana kuja kuwekeza hapa nchini katika sekta mbalimbali zikiwemo Mafuta na gesi, Kilimo, Uvuvi, Mbuga za wanyama, Madini na ufugaji.

Amesema hivi sasa Tanzania ipo katika mpango wa ujenzi wa viwanda na pia inatekeleza mpango wa pili wa maendeleo, hivyo amemuomba Balozi wa Ukraine hapa nchini awahamasishe wafanyabiashara na wawekezaji wa Ukraine waje kuwekeza katika viwanda kwani soko la uhakika la bidhaa lipo.

Rais Magufuli pia amewasihi Mabalozi wa Slovakia, Ukraine na Ghana ambao makazi yao ya Ubalozi yapo Mjini Nairobi nchini Kenya kuanzisha Ubalozi wao hapa nchini ili kuimarisha zaidi uhusiano na ushirikiano katika masuala ya biashara na uwekezaji.

Lionel Messi Kuwakabili Deportivo La Coruna
Riyad Mahrez: Leicester City Walinizuia Nisiende Arsenal