Kamati Maalumu iliyoundwa na Wabunge wa Bunge la Afrika (Pan- African Parliament – PAP) imetoa ripoti ya uchunguzi dhidi ya Rais wa Bunge hilo, Roger Nkodo Dang.

Nkodo anatuhumiwa kwa unyanyasi wa kingono kwa watumishi wa kike walioko Makao Makuu ya PAP, matumizi mabaya ya madaraka, upendeleo ndani ya bunge hilo na unyanyasaji kwa watumishi wa ofisi hiyo hali iliyosababisha kuwepo kwa mgomo wa watumishi wiki iliyopita.

Mwenyekiti wa Kamati hiyo Maalumu ya Uchunguzi, Jaji Mstaafu wa Mahakamani Kuu ya Kenya, Stewart Madzayo ametoa ripoti hiyo leo jioni katika kikao cha bunge kikiongozwa na Makamu wa nne wa rais wa Bunge la Afrika, Chief Charumbira.

Aidha, ripoti ya kamati hiyo imeonyesha kuwa Rais wa PAP, Nkodo Dang amekutwa na kesi ya kujibu na hivyo wabunge wameazimia kuikabidhi Umoja wa Mataifa (AU) kwa ajili ya uchunguzi wa kina (forensic investigation) ambapo Rais huyo ametakiwa apishe ili uchunguzi uweze kufanyika.

Akizungumza na waandishi wa habari, baada ya kutoka kwenye kikao cha bunge ambacho waandishi wa habari hawakuruhusiwa kuingia, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Bunge la Afrika, Stephen Masele amesema Kamati hiyo imefanya kazi nzuri.

“Kwanza Nimefurahi kwamba Kamati Maalumu iliyoundwa na Bunge kuchunguza tuhuma dhidi ya rais wa PAP anazotuhumiwa imefanya kazi vizuri, na mimi kama mkuu wa Utawala wa Bunge la Afrika na wafanyakazi wote wa PAP, nina wajibu wa kuhakikisha kwamba haki za wafanyakazi hususani wanawake ambao wanamtuhumu rais kwa kuwanyanyasa kingono zinalindwa, amesema Masele.

Hata hivyo, ameongeza kuwa utafiti wa kamati umethibitisha kuwa alifanya hivyo na yeye mwenyewe amekiri kuwa alifanya na ameomba msamaha, huku bunge limeazimia asimamishwe kupisha Umoja wa Afrika ufanye uchunguzi wa kina.

Membe amjibu Rostam kuhusu kugombea 2020, 'sote tumekatwa mikia'
Video: Fahamu utamaduni wa kumkata kidole mwanamke aliyefiwa