Wizara ya Sheria ya Marekani juzi ilimtaja mpelelezi wa zamani wa uhalifu wa kivita kama wakili maalumu wa kusimamia uchunguzi wa uhalifu, dhidi ya Donald Trump, siku tatu baada ya rais huyo wa zamani kutangaza kuwa atagombea tena uchaguzi wa rais wa mwaka 2024.

Trump, ambaye anadai kuwa ‘anawindwa na wachawi’, alikashifu hatua hiyo akisema isiyo ya haki na siasa chafu katika nchi yao huku Ikulu ilikanusha uingiliaji wa kisiasa, lakini uchunguzi wa mawakili maalumu wa Rais wa zamani na mgombea wa sasa unaweka mazingira ya vita vya kisheria.

Katika mkutano na waandishi wa habari, Mwanasheria Mkuu Merrick Garland alitangaza uteuzi wa Jack Smith, ambaye alikuwa mwendesha mashtaka mkuu huko The Hague, akichunguza uhalifu wa kivita wa Kosovo, kuchukua jukumu la chunguzi mbili zinazoendeshwa dhidi ya Trump.

Donald Trump ametangaza tena kuwa atagombea urais wa Marekani mwaka 2024. Picha ya CNN.

Uchunguzi mmoja unaangazia juhudi za Rais huyo wa zamani za kutengua matokeo ya uchaguzi wa 2020 na shambulio la Januari 6, 2021 dhidi ya Ikulu ya Marekani lililofanywa na wafuasi wake.

Nyingine ni uchunguzi wa hifadhi ya nyaraka za siri za Serikali zilizonaswa wakati Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI) lilipovamia kwenye makazi ya Trump ya Mar-a-Lago huko Florida Agosti mwaka huu.

Mwanasheria Garland alisema kumtaja wakili maalumu ni kwa manufaa ya umma kwa sababu Trump wa chama cha Republican na mrithi wake wa Chama cha Democratic, Joe Biden wameeleza nia yao ya kugombea 2024, ingawa ni Trump pekee ndiye ametangaza rasmi kwa sasa.

Waziri awahakikishia Wadau mabadiliko sheria ya Habari
Obiang atarajia ushindi baada ya utawala wa miaka 43