Mkuu wa Mkoa wa Songwe Brigedia Jenerali Nicodemas E Mwangela amekataa ombi la Mkandarasi kutoka kampuni ya Mats Engineering Ltd Paulo Philipo Paulo la kuongezewa kipindi cha miezi miwili ili aweze kukamilisha ujenzi wa Daraja la Kikamba Wilayani Songwe.

Brigedia Jenerali Mwangela amekataa ombi hilo mara baada ya kufanya ukaguzi wa ujenzi wa daraja la Kikamba linalounganisha kata za Kapalala na Gua wilayani Songwe kwakuwa sababu alizotoa mkandarasi huyo hazijitosheleji.

Amesema daraja hilo lazima likamilike kwa muda uliopangwa ambao ni Septemba, 2018 huku mkandarasi huyo akitoa sababu kuwa atachelewa kukamilisha ujenzi huo kutokana na mvua nyingi zilizonyesha na mwamba mgumu uliopo eneo la ujenzi.

“Mkandarasi ahakikishe anafanya kazi mchana na usiku ili akamilishe ndani ya muda wa mkataba, vifaa vya kumuwezesha kufanya hivyo anavyo na ombi la kuongezewa muda wa ujenzi mimi siafikiani nalo”, amesema Brigedia Jenerali Mwangela.

Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Songwe, Samuel Jeremia amesema kuwa yeye na viongozi wengine wataendelea kusimamia miradi ya maendeleo na katika ujenzi wa daraja hilo watahakikisha wanamsimamia mkandarasi huyo ili amalize ndani ya muda uliopangwa.

Hata hivyo, daraja la Kikamba linaolunganisha kata za Kapalala na Gua limeanza kujengwa mwezi Oktoba 2017 na linatarajiwa kukamilia Septemba 2018 likiwa limegharimu shilingi bilioni 1.4.

Kevin de Bruyne hatarini kuikosa Manchester derby
NEC yaujibu ubalozi wa Marekani, yautaka utoe uthibitisho