Mwenyekiti wa Hamasa na Chipukizi (UVCCM) mkoa wa Njombe, Issabela Mgimba ameipongeza Serikali mkoani humo kufuatia hatua zilizochukuliwa na vyombo vya dola kwa kuwakamata na kuwachukulia hatua za kisheria wote waliojihusisha na mauaji ya watoto wadogo mkoani Njombe.

Ametoa pongezi hizo mbele ya katibu wa NEC, Uchumi na Fedha (CCM) Taifa, Dkt. Frank Hawassi alipokutana na viongozi mbalimbali wa chama na serikali ambapo amesema kuwa watoto wote wa mkoa wa Njombe sasa wana amani baada ya wahusika wa matukio hayo kukamatwa.

‘’Ndugu mgeni Rasimi sisi watoto wa mkoa wa Njombe tuna ipongeza sana serikali ya mkoa wetu ikiongozwa na mkuu wa mkoa wetu, Christopher Ole Sendeka kwa kutambua haki na uhuru wa kumlinda mtoto kwa kupambana na wahalifu hao,” amesema Issabela

Aidha, Katibu wa NEC, Uchumi na Fedha wa Chama cha Mapinduzi CCM, Dkt. Hawassi amewahakikishia usalama watoto wote nchini kwakuwa chama kinaendelea kuisimamia Serikali kuhakikisha inatekeleza majukumu yake ikiwemo kulinda usalama wa watoto na Watanzania wote.

Kwa upande wake kaimu mkuu wa mkoa wa Njombe ambaye ni mkuu wa wilaya ya Njombe, Ruth Msafiri akiwa wilayani Ludewa amewaeleza wananchi wote wa mkoa huo kuwa tayari wahusika wa mauaji hayo wamekamatwa na kesi zao zimeshaanza kutajwa mahakamani.

 

Manispaa ya Iringa yaongoza kwa ukusanyaji mapato
Serikali yalaani vikali mauaji ya watoto