Mbunge wa Chalinze, Ridhiwani Kikwete ambaye pia ni mtoto wa Rais wa awamu ya nne, Dkt. Jakaya Kikwete amesema kuwa anaona mabadiliko ya namna watu wanavyomchukulia, tofauti na ilivyokuwa wakati familia yake iko Ikulu.

Akizungumza kwenye mahojiano maalum na Dar24 ndani ya eneo la Bunge jijini Dodoma, Ridhiwani alisema kuwa mengi yalizushwa kuhusu yeye hasa ya umiliki wa mali nyingi kwa sababu ambazo hazifahamu, lakini anaamini kulitokana na yeye kuwa mtoto wa Rais.

Mbunge huyo wa Chalinze ambaye aliwahi kutungiwa wimbo na Izzo Bizness akimtaka ‘aongee na baba yake’ kuhusu changamoto za maisha ya vijana mtaani, ametaja hali ya kuzushiwa kumiliki vitu vya thamani karibu vyote nchini kuwa moja kati ya changamoto alizokuwa anazipata kwa kuwa mtoto wa Rais.

“Hata wakati mwingine kuna mambo yanafanyika, hata huyajui, hata hujashiriki… unajua kuna mambo mengine unaweza kuwa hapa unaongea na vyombo vya habari, kesho unakuja kuambiwa labda ‘ile Dar24 ya kwako Ridhiwani’! Unaweza kudhani labda walivyoona mimi nahojiwa wanaweza kudhani labda ila Dar24 ya kwangu,” alisema.

“Mengi sana yamesemwa, maasasi ya kwangu, Oilcom, Camel Oil… mashirika mbalimbali yanatajwa, lakini sasa hivi kelele zile hakuna tena,” aliongeza.

Ridhiwani amesema kuwa tofauti na ilivyokuwa wakati ule, hivi sasa anataswira tofauti kwa watu wengi zaidi kwenye jamii kama kiongozi anayewatetea wananchi na kutatua kero zao, akiwa huru zaidi kama mwanasiasa.

Kama ilivyo kwa baba yake, Mbunge huyo amesema kuwa hupenda ‘kujichanganya’ na watu wa aina mbalimbali na kufanya mazungumzo ya kawaida na watu wake kuhusu mpira pamoja na yale yanayohusu ujana.

Angalia video hii kupata undani wa mahojiano yake:

Mwarabu Fighter amvuruga Zola D, ‘mimi ni mwalimu wako’
Njia asili za kuondoa weusi kwapani na mapajani