Hatimaye msanii Roma Mkatoliki akiwa na wenzake watatu amezungumza na vyombo vya habari kwa mara ya kwanza kufuatia tukio la kutekwa na watu wasiojulikana kwa takribani siku tatu.

Roma na wenzake wamejitokeza mbele ya vyombo vya habari baada ya kutoka katika hospitali ya Mwananyamala jijini Dar es Salaam, walikoenda kupimwa afya zao baada ya kuhojiwa kwa takribani saa sita katika kituo cha polisi cha Oysterbay.

Msanii huyo amewashukuru watanzania kwa ushirikiano wao waliouonesha na kuwahakikishia kuwa wako salama kiafya. Alisema ingawa hajaingia kwenye mitandao lakini ameelezwa juhudi zilizofanywa na watanzania.

“Niwahakikishie mimi ni mzima kabisa mpaka sasa hivi, niko salama kiafya na hata kiakili. Na hata wenzangu watatu, Moni, Laden na Imma… niwahakikishie kabisa kuwa sisi wote ni wazima na tunaendelea vizuri,” alisema Roma na kuomba wapewe nafasi kwanza wakapumzike.

Aliongeza kuwa kwa sasa wako katika taratibu za kuelezea vyombo vya usalama kuhusu tukio zima la kutekwa kwao hivyo hawawezi kuweka wazi kwa umma kwa sasa.

Aidha, Roma ameahidi kuwa siku ya Jumatatu watazungumza na vyombo vya habari na kuueleza umma kuhusu undani wa kilichojili.

Roma na wenzake walitekwa na watu wasiojulikana katika studio za Tongwe Records ambapo watu hao walichukua pia vifaa vya studio hiyo ikiwa ni pamoja na ‘computer’ na runinga bapa, kwa mujibu wa mmiliki wa studio hizo.

Nape asema kinachoendelea kwa sasa sio sahihi
Diamond Amuangukia Gwajima, ‘Mzee Wangu Usinigeuze Maji’