Wachezaji Cristiano Ronaldo, Lionel Messi, Eden Hazard na Kylian Mbappe wametajwa kuwa miongoni mwa wanaounda kikosi bora cha FIFA kwa mwaka 2017/18.

Orodha ya wachezaji 11 wanaounda kikosi hicho ilitajwa usiku wa kuamkia leo, katika hafla ya utoaji tuzo ya mchezaji bora wa dunia wa FIFA iliyofanyika jijini London.

Mchezaji mwingine aliyewastaajabisha wadau wengi wa soka kwa kuingia kwa mara ya kwanza kwenye kikosi hicho, ni kiungo wa klabu ya Chelsea na timu ya taifa ya Ufaransa N’Golo Kante.

Kante amefanikiwa kutajwa kwenye kikosi hicho, kufautia umahiri wake wa kusakata soka akiwa na klabu ya Chelsea na timu yake ya taifa, jambo ambalo kila mmoja amekua akilikubali kila kukicha.

Baada ya kutangazwa kuingia kwenye orodha hiyo Kante alisema, nimefarijika kuwa miongoni mwa wachezaji wanaounda timu hii, ni heshima kwangu, nimefurahi sana.”

Hata hivyo, mshangao mkubwa kwa wadau wengi wa soka ulisababishwa na kutokuwepo kwa mshambuliaji wa Misri na klabu ya Liverpool Mohamed Salah, kwenye kikosi hicho.

Salah alitarajiwa kuwa miongoni mwa wachezaji waliotajwa, baada ya kutangazwa kuwa mshindi wa tuzo ya bao bora ya mwaka, lakini haikua hivyo.

Mwingine ambaye ameachwa katika kikosi hicho licha ya kutajwa kama mshindi wa tuzo usiku wa kuamkia leo, ni mlinda mlango Thibaut Courtois (Mlinda mlango bora wa mwaka), na nafasi ya mlinda mlango kwenye orodha iliyotajwa ilikwenda kwa mlinda mlango wa klabu ya Manchester United na Hispania David de Gea.

Orodha ya kikosi bora cha FIFA mwaka 2017/18.

  1. David de Gea – Manchester United na Hispania
  2. Dani Alves – PSG na Brazil
  3. Rafael Varane – Real Madrid and France
  4. Sergio Ramos – Real Madrid na Hispania
  5. Marcelo – Real Madrid na Brazil
  6. Luka Modric – Real Madrid na Croatia
  7. N’Golo Kante – Chelsea na Ufaransa
  8. Eden Hazard – Chelsea na Ubelgiji
  9. Lionel Messi – Barcelona na Argentina
  10. Kylian Mbappe – PSG na Ufaransa
  11. Cristiano Ronaldo – Real Madrid/Juventus na Ureno

 

Wanawake kuwania Ballon d'or
Rais awashika mkono wafiwa, manusura MV Nyerere, walamba mamilioni