Rosa Ree amefunguka kuhusu mistari ya wimbo wa rapa mwenzake wa kike, Chemical inayoaminika kuwa ni kombora lililorushwa kwake pamoja na rapa mwingine wa kike, Tammy The Baddest.

Mkali huyo wa mashairi na mitindo amefunguka kupitia The Playlist ya Times FM ambapo amewataka wasanii wa kike kujikita katika kusaidiana na kushikana mkono ili wafike mbali zaidi kuliko kushambuliana.

“Wanachanachana tu hawa Goddess, ahah- eti Mabaddest

Mi nachana bure and I get this, sifanye kwa fame…” alisikika Chemical kwenye ‘Jipange aliyomshirikisha Mr. Blue. Rosa Ree hujiita ‘The Goddess na Tammy ni ‘The Baddest’.

The Goddess wa rap, awali alimtaka mtangazaji Lil Ommy alielekeze swali la kueleza maana ya mistari hiyo ya Chemical kwa muandishi wa mashairi, lakini baadaye aliamua kutoa ushauri na muongozo pia.

“Mimi nahitaji jamii ambayo tunainuana kuliko kupeana madongo. Ukijaribu kumzima mwenzako hauwezi kuwaka zaidi,” alifunguka Rosa Ree.

Alisisitiza kuwa Bifu sio kitu anachokiamini na kwamba daima hawezi kujiingiza kwenye bifu ya aina yoyote.

Hata hivyo, Rosa Ree alibanwa na swali lingine kuwa mashabiki wanaamini alimjibu Chemical kwenye wimbo wake wa ‘Pochi Nene’, alipodai kuwa “siwezi kuimba visingeli”. Mtazamo huu ulikuja kwakuwa mbali na kurap, Chemical amewahi kuimba wimbo wenye muelekeo wa Singeli.

“Kwani yeye anaimba visingeli? Aliuliza Rosa Ree. “Kuna watu wengi sana naamini wanaimba Singeli kama akina Msaga Sumu… hao muziki huo ni wa kwao na sio aina ya muziki wangu. Kwahiyo, mimi na mtu anayefanya Singeli hatuwezi tukafanana,” alifunguka akichanganya mara  Kiswahili na lugha ya kigeni ya ardhi ya Malkia.

The rap Goddess hivi karibuni ameingia mkataba na menejimenti mpya ambayo imempa neema nzito ya pesa na majumba mawili ya kifahari. jumba moja lina thamani ya sh400 milioni ambalo amedai liko nchini Tanzania na jingine liko nchini Afrika Kusini.

‘Way Up’ ndio wimbo mpya na wa kwanza kutoka kwa Rosa Ree akiwa chini ya usimamizi wa kampuni mpya ya Afrika Kusini. Rapa Emtee wa Afrika Kusini amefanya yake pia kwenye wimbo huo.

Wabunge wazibwa midomo kuhusu Trilioni 1.5
Suti ya Sugu yazua utata Bungeni