Klabu ya Swansea City inajipanga kufanya mazungumzo na aliyekua meneja msaidizi wa Man Utd Ryan Giggs.

Gazeti la The Telegraph mapema hii leo limeibuka na taarifa za klabu hiyo ya mjini Swansea, kuanza kumsaka mbadala wa Francesco Guidolin ambaye aliajiriwa Mwezi Januari mwaka huu kama mbadala wa Garry Alan Monk.

Guidolin ambaye ni raia wa Italia, ameanza vibaya msimu huu wa ligi, jambo ambalo limeibua hisia mbaya kwa viongozi wa Swansea City ambao wanataka kuona klabu yao inafanya vyema kama ilivyokua misimu mitatu iliyopita.

Jina la Giggis linadaiwa kutajwa sana na viongozi hao, kwa kuamini huenda akawa mtu sahihi wa kumaliza tatizo la mwenendo mbaya unaowakabili kwa sasa, na wamedhamiria kuuepuka mtihani huo kabla ligi haijachanganya.

Giggs mwenye umri wa miaka 42, aliamua kuondoka Old Trafford, siku chache baada ya uongozi wa Man Utd kuthibitisha mpango wa kumpa ajira Jose Mourinho, na baadae ilibainika gwiji huyo alikuwa akihitaji nafasi ya kuwa meneja mkuu klabuni hapo kufuatia kuondoka kwa Louis Van Gaal.

Giggs alianza shughuli za kusaidia benchi la ufundi wakati wa utawala wa David Moyes na meneja huyo alipotimuliwa siku kadhaa kabla ya kumalizika kwa msimu wa 2013/14, uongozi wa Man Utd ulimkabidhi jukumu la kukiongoza kikosi na baadae ulimuajiri Van Gaal.

Serengeti Boys Yaenda Kigali - Rwanda
Ljungberg: Wenger Amepata Dawa Ya Kumaliza Ukame