Msichana anayetuhumiwa kushambulia kwa risasi ofisi za makao makuu ya YouTube zilizoko California nchini Marekani, anadaiwa kuwa alifanya hivyo akiwa na hasira dhidi ya kampuni hiyo.

Ripoti ya awali ya polisi kuhusu tukio hilo imeeleza kuwa Nasim Aghdam mwenye umri wa miaka 39, alifyatua risasi na kuwajeruhi watu wawili nje ya ofisi hizo na baadaye kujiua, Jumanne wiki hii kutokana na mengi aliyokuwa amekwishayasema mtandaoni.

Polisi wameeleza kuwa mwanamke huyo alikuwa akiilaumu YouTube kwa kile alichodai kumbania video zake na kumkosesha watazamaji wengi, hatua inayomfanya kutoingiza kiasi cha fedha anachostahili.

Vyombo vya habari vya Marekani vimeeleza kuwa Nasim alikuwa anamiliki akaunti/channel maarufu ya YouTube pamoja na tovuti na kwamba alikuwa akijitanabaisha kama msanii wa hip hop na mbeba vitu vizito. Akaunti zote zimefutwa.

Januari mwaka jana, Nasim anadaiwa kuweka kwenye akaunti/channel yake ya YouTube kipande cha video kinachomuonesha akilalamika kuwa YouTube wamekuwa wakimfanyia ‘figisu’ za kumkosesha watazamaji wengi na kuchakachua video anazoweka.

Watu wanaoweka video YouTube wanaweza kupokea fedha kutoka kwenye kampuni hiyo lakini kampuni hiyo inaweza kupunguza kipato cha mwenye channel/akaunti kwa sababu mbalimbali ikiwa ni pamoja na kwenda kinyume na sera zake.

 

Nondo kuteta na IGP, DCI na AG Mahakamani
Miili ya Wanajeshi wa Uganda yawasili nchini humo