Mamlaka ya Udhibiti wa Manunuzi ya Umma (PPRA), imewataka wananchi kuendelea kutembelea banda lao katika Maonesho ya 43 ya Kimataifa ya Biashara maarufu kama Sabasaba yanayofanyika jijini Dar es Salaam, ili kupata elimu ya sheria na Mfumo wa Manunuzi kwa Njia ya Mtandao (TANePS).

Afisa Mtendaji Mkuu wa PPRA, Mhandisi Leonard Kapongo ambaye alikuwa kwenye banda hilo Julai 3, 2019, aliwaambia waandishi wa habari kuwa Mamlaka inaendelea kusimamia Sheria ya Manunuzi ya Umma ya Mwaka 2011 iliyofanyiwa marekebisho mwaka 2016 ili kuhakikisha kuwa manunuzi yanayofanywa yanazingatia thamani halisi ya fedha.

Aidha, aliwataka wananchi kushirikiana na Mamlaka kutoa taarifa kuhusu ukiukwaji wa sheria ya manunuzi ya umma na kwamba wahusika watachukuliwa hatua.

Afisa Mtendaji Mkuu wa PPRA, Mhandisi Leonard Kapongo akizungumza na wafanyakazi wa Mamlaka hiyo kwenye Maonesho ya 43 ya Kimataifa ya Biashara maarufu kama Sabasaba, jijini Dar es Salaam

Mhandisi Kapongo alisema kuwa uzingatiaji wa Sheria ya Manunuzi ya Umma ni nyenzo ya kudhibiti matumizi ya fedha za umma katika kuhakikisha kuwa fedha zilizotolewa kwa ajili ya maendeleo zinatumika kama zilivyokusudiwa ili kufikia malengo ya kuwa nchi yenye uchumi wa kati na kuboresha maisha ya Watanzania.

Katika maonesho hayo, PPRA inatoa elimu kuhusu Mfumo wa Manunuzi ya Umma kwa Njia ya Mtandao (TANePS), ambao unalenga katika kuongeza uwazi na uwajibikaji katika michakato yamanunuzi nchini.

Kwa mujibu wa Mamlaka, wazabuni 1,958 wameshajiandikisha katika TANePS. Wazabuni hao ni kutoka katika mikoa mitano iliyofanyiwa majaribio katika Mwaka wa Fedha 2018/19. Mikoa hiyo ni Dar es Salaam, Dodoma, Arusha, Mwanza na Mbeya.

Video: Kitendawili uchaguzi kujaza nafasi ya Lissu, CAG atoa mbinu vita dhidi ya Rushwa
Boeing kutoa dola milioni 100 kwa waathirika wa ajali za ndege Ethiopia na Indonesia