Mbunge wa Mchinga (CUF), Hamidu Bobali amesema uamuzi wa Chuo Kikuu Dar es salaam (UDSM) kumsimamisha masomo mwanafunzi wake wa mwaka wa tatu, Abdul Nondo hayakuwa maamuzi sahihi kwani umekitia aibu chuo hicho pia ni kinyume na haki za binadamu.

Bobali amehoji ni wanafunzi wangapi ambao kesi zao zipo mahakamani lakini wanaendelea na masomo.

”Hili suala la Nondo linakitia aibu chuo pengine watueleze tu kwamba jambo hili ni la kisiasa” amehoji Bobali.

Wakati Bobali akitoa maelezo hayo, mbunge wa Magogoni CUF, Dk Ally Yusuf Suleiman aliomba taarifa kwa Mwenyekiti wa Bunge, Andrew Chenge na kubainisha kuwa hata wabunge wapo walioshtakiwa, wengine kufungwa lakini mpaka sasa bado wanaendelea na ubunge wao.

”Napenda kumpa taarifa mzungumzaji (Bobali) kuwa hata wabunge wapo walioshtakiwa lakini mpaka kufungwa lakini bado ni wabunge hadi sasa,” amesema Suleiman.

Nondo ambaye ni mwenyekiti wa Mtandao wa Wanafunzi Tanzania (TSNP) amesimamishwa masomo kuanzia Machi 26, 2018 kwa barua iliyoandikwa na Makamu Mkuu wa Chuo hicho, Profesa William Anangisye aliyemsimamisha kwa taratibu za chuo.

Nondo anakabiliwa na kesi ambapo kesi yake bado inasikilizwa mahakamani, anashitakiwa kwa tuhuma mbili, ya kwanza ikiwa ni kutumia vibaya mtandao wa kijamii kwa kusambaza taarifa za uongo kuwa ametekwa, kosa la pili likiwa ni kudanganya polisi alipofika kituo cha polisi Iringa kuwa alitekwa huku taarifa zikidai kuwa alienda Mafinga kumsalimia mpenzi wake.

Iran yazikana nyaraka za Israel, yasema ni za uchochezi
Kamati ya Bunge yapinga kuhamishwa kwa Walimu