Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Bw. Evarist Ndikilo atoe wiki mbili kwa wakuu wa taasisi za umma na za binafsi wajieleze ni lini wataendeleza viwanja vya ofisi walivyopewa mjini Kibaha.

Ametoa agizo hilo leo Septemba 21, 2016 wakati akizindua Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania (2015 – 2020) na Mradi wa Maboresho ya Mahakama ya Tanzania, Kibaha, mkoani Pwani.

Waziri Mkuu ametoa agizo hilo baada ya kupokea malalamiko kutoka kwa Mkuu wa Mkoa huo kwamba kuna taasisi za umma na za binafsi ambazo zimepewa viwanja vya kujenga Ofisi kwa zaidi ya miaka mitatu lakini zimeshindwa kuviendeleza hadi sasa wakati kuna watu bado wana shida ya kupatiwa viwanja.

“Kibaha ni kimbilio la mkoa wa Dar es Salaam, kule kumejaa na hapa kuna nafasi kwa hiyo hawa ambao hawajaendeleza waandikie barua leo hii hii na uwape wiki mbili waeleze ni lini watakuwa tayari kuanza kazi hiyo.” – Majaliwa

Taasisi hizo zilizotanjwa na Waziri Mkuu ni Hazina ndogo yenye viwanja viwili ambapo kiwanja kimoja chenye namba 232 kimeendelezwa lakini kiwanja kingine chenye namba 221 bado hakijaendelezwa. Taasisi nyingine na viwanja vyao kwenye mabano ni Chuo Kikuu Huria (kitalu na. 228), Njuweni Institute (kitalu na. 229), TANESCO (kitalu na. 218), TRA (kitalu na. 233) na SF Group (kitalu na. 225). Vingine ni vya Benki ya CRDB na TAKUKURU ambavyo hakutaja namba za vitalu vyake.

Majaliwa amesema kuwa anajua kuna watu wa Serikali watasema hawana bajeti, lakini Bunge la bajeti linaanza Aprili mwakani. Kwa hiyo, wajipange kwenye bajeti ijayo, ili ifikapo Julai mosi, 2018 hawajafanya kitu, wachukuliwe hatua.

“Tuchukue viwanja vyetu tuwape wengine, na hawa wanaosuasua, tuwaache ili watakapokuwa tayari waombe upya na tutawapa wakati mwingine,” Majaliwa.

Waziri Mkuu pia amemtaka Ndikilo awawekee deadline ya kujieleza katika barua hizo.

Michezo Ya Simba, African Lyon Yarejeshwa Uwanja Wa Taifa
Audio: Kamanda Msangi atoa taarifa ya ajali ya Basi la Super Shemi