Nahodha na mshambuliaji wa kikosi cha taifa Stars Mbwana Ally Samatta amewapongeza wachezaji wa timu hiyo, kwa kufanikisha lengo la kufuzu fainali za mataifa bingwa ya Afrika “CHAN” kwa kuifunga Sudan mabao mawili kwa moja mjini Khartoum, jana usiku.

Samatta ambaye hakuwepo kikosini hiyo jana kufuatia kanuni za michuano ya CHAN kumnyima nafasi ya kushiriki, ametoa pongezi hizo kupitia ukurasa wake wa mtandao wa kijamii wa Twitter.

Kanuni za michuano ya CHAN zinawabana wachezaji wanaocheza nje ya ligi za nyumbani kwao kushiriki kwenye vikosi vyao, kwa kusudio la kuwapa fursa wachezaji wanaocheza ligi za ndani, kuonekana kimataifa.

Mshambuliaji huyo ambaye anaitumikia klabu ya KRC Genk ya Ublegiji ameandika, “Heshima kubwa mmetupa watanzania, nasimama kwa heshima, navua kofia yangu nawapigia saluti ya heshima, asante sana @TaifaStars na hongereni kwa kufuzu kwenye michuano ya CHAN 2020, na kama ilivyo ada basi hapo hapo Sudan anzeni kunywa izo koka bili juu yangu.”

Taifa Stars imefanikiwa kukata tiketi ya kucheza fainali za mataifa bingwa barani Afrika “CHAN” kwa kubebwa na kanuni ya bao la ugenini.

Kimtazamo matokeo ya jumla baina ya Taifa Stars dhidi ya Sudan ni mabao mawili kwa mawili, lakini Tanzania imefanikiwa kufunga mabao mawili katika uwanja wa ugenini, tofauti na ilivyokua kwa wapinzani wao waliopata bao moja katika mchezo wa mkondo wa kwanza uliopigwa jijini Dar es salaam mwishoni mwa mwezi uliopita.

Shujaa wa Taifa Stars katika mchezo wa jana alikuwa mshambuliaji Ditram Nchimbi aliyeongezwa kikosini baada ya mchezo wa mkondo wa kwanza, ambaye alisababisha bao la kwanza na kufunga la pili.

El Clasico kurindima Disemba 07
Habari kubwa katika Magazeti ya Tanzania leo Oktoba 19, 2019