Saudi Arabia imezipinga ripoti zinazodai kwamba CIA imesema kuwa Mwanamfalme, Mohammed bin Salman ndiye aliyetoa maagizo ya kuuawa kwa mwandishi wa habari, Jamal Khashoggi katika ubalozi mdogo wa Saudia nchini Uturuki.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Saudi Arabia, Adel al Jubeir amezipinga ripoti zinazosema kwamba mwandishi huyo wa habari, Jamal Khashoggi raia wa Saudi Arabia aliyeuawa katika ubalozi mdogo wa nchi hiyo nchini Uturuki aliuawa kwa maagizo ya Mwanamfalme Mohammed bin Salman.

Amesema kuwa ufalme wa Saudia unajua kwamba madai hayo kuhusu mwanamfalme hayana ukweli na wanayapinga kikamilifu na hawatoruhusu katu majaribio ya kuuhujumu uongozi wa taifa hilo kwa namna yoyote na kutoka kwa mtu yoyote.

Aidha, ameongeza kuwa haki katika tukio la kuuliwa Khashoggi ni kitu cha kwanza ambacho Saudi Arabia inakitaka kabla hata ya Jumuiya ya kimataifa kuishinikiza haki hiyo.

“Saudi Arabia itaendelea kukabiliana na itikadi kali na ugaidi na tutasimama imara dhidi ya kundi linalojaribu kuiteka dini yetu ya kweli. tutaendelea kubeba jukumu la uongozi na kuleta maendeleo katika ukanda huu na hivyo basi kuongeza fursa za uwekezaji kikanda na kimataifa.”amesema Adel al Jubeir

Hata hivyo, nchi za Ulaya, Ufaransa na Ujerumani zimejitokeza waziwazi na kusema kuwa zitaiwekea vikwazo Saudi Arabia.

 

Video: Tume ya Taifa ya Umwagiliaji yatakiwa kuhakiki eneo linalofaa kwa kilimo
Liverpool kutia mkono kwa Kalidou Koulibaly