Serikali kupitia Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA) imejizatiti kupanua wigo na kuboresha huduma za hifadhi ya jamii hasa kwa kundi la watu walio kwenye sekta isiyo rasmi.

Hayo yamebainishwa na Mkurugenzi wa Sheria kutoka Mamlaka ya Usimamizi na Udhibiti wa Sekta ya Hifadhi ya Jamii (SSRA), Bw. Onorius Njole wakati  akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam kuhusu Mpango Maalum wa kutoa huduma ya hifadhi ya jamii kwa sekta isiyo rasmi maarufu kama Informal Sector Scheme ambayo inajumuisha waendesha bodaboda, bajaji na mama lishe.

Bw. Njole alisema kuwa katika kuhakikisha watanzania wote wananufaika na huduma za hifadhi ya jamii, SSRA inafanya tafiti mbalimbali na kuhamasisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kubuni mafao mbalimbali yanayolenga kuwafikia wananchi wote walio kwenye sekta isiyo rasmi.

Ili kufanikisha hilo, mwaka 2015 SSRA ilifanya utafiti katika sekta ya usafirishaji na kubaini kuwa asilimia 83 ya waendesha vyombo vya usafiri mijini wakiwemo waendesha bodaboda wako tayari kuchangia kwa hiari katika Mifuko ya Hifadhi ya Jamii.

“Kutokana na matokeo hayo mamlaka ilipendekeza kuanzishwa kwa Mpango Maalum ujulikanao kama Informal Sector Scheme ambapo watu waliojiajiri kwenye sekta isiyo rasmi watapata nafasi ya kunufaika na huduma ya hifadhi ya jamii.” Alisema Njole.

Njole aliongeza kuwa tayari baadhi ya mifuko imekwishaandaa mafao maalum yanayowalenga waendesha bodaboda, bajaji, daladala na mama lishe ambao watapata fursa ya kuchangia kiasi kidogo kila siku kulingana na kipato chao ili kupata huduma za hifadhi ya jamii kama vile akiba ya uzeeni, matibabu na mikopo.

Aidha, Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Uhamasishaji wa SSRA, Bi. Sarah Kibonde alieleza kuwa mamlaka hiyo inaendelea na zoezi la kutambua na kusajili Mifuko yote ya Bima ya Afya ya Jamii (CHFs) kwa lengo la kuboresha huduma na kuimarisha mfumo wa utoaji huduma za afya kwa wananchi.

Pia Bi. Sarah alisema kuwa SSRA imeandaa program maalum kwa ajili ya kutoa elimu ya hifadhi ya jamii kwa Wakurugenzi wa Halmashauri na Waratibu wa Mifuko ya Bima ya Afya ya Jamii nchini kote na zoezi hilo linaenda sambamba na usajili wa mifuko hiyo kwa mujibu wa Sheria ya SSRA, Sura ya 135.

“Program hii imeanzia Kanda ya Kati ambako ilihusisha Wilaya 27 na jumla ya CHF 5 zilisajiliwa na nyingine 22 zinakamilisha taratibu za usajili. Zoezi hili linatarajiwa kuendelea Juni 22 kwa mikoa ya Nyanda za Juu Kusini ambako jumla ya CHF 25 zinatarajiwa kusajiliwa.”

Sambamba na program hiyo Serikali kupitia Wizara ya Afya na Wizara yenye dhamana ya masuala ya hifadhi ya jamii na SSRA inafanya mapitio ya mfumo wa usimamizi wa Mifuko ya Bima ya Afya ya Jamii (CHF) ili kupata mfumo utakaoweza kutoa huduma ya afya kwa watanzania wote

Huduma ya Chakula Muhimbili Kwa Wagonjwa Kuanza Agost 1
Nisha kufturu pamoja na watoto waishio kwenye mazingira magumu Dar.