Timu ya Taifa ya Mpira wa Miguu ya vijana wenye umri wa chini ya miaka 17 – Serengeti Boys, imeanza rasmi kambi ya wiki moja kabla ya kwenda Korea Kusini ambapo itashiriki michuano maalumu ya kimataifa iliyoandaliwa na Shirikisho la soka Korea Kusini.

Timu hiyo itapiga kambi kwa wiki moja kwenye Hosteli za TFF zilizopo Uwanja wa Kumbukumbiu ya Karume, Ilala jijini Dar es Salaam. Tayari vijana wameripoti kwenye hosteli hizo tangu jana Oktoba 31, 2016.

Ikiwa Korea, itashiriki michuano hiyo kwa siku takribani 10 kabla ya kurejea nchini ambako itapangiwa programu nyingine ikiwa ni kucheza na nyota 40 walioteuliwa na Airtel baada ya michuano ya Kampuni hiyo ya simu iliyofanyika mwaka huu kwenye kona mbalimbali nchini kabla ya fainali zake kufanyika Uwanja wa Karume, Dar es Salaam.

Serengeti Boys imepata nafasi hiyo kutokana na umahiri wake wa kucheza soka la ushindani, kwani kwa kipindi cha mwaka mmoja tu, imeweza kucheza michezo 16 ya kimataifa ambapo imekuwa ikifanya vema katika mechi 15 kabla ya 16 iliyopoteza dhidi ya Congo-Brazaville katika michuano ya kuwania nafasi ya kucheza Kombe la Mataifa ya Afrika.

Raundi Ya 14 Ligi Kuu Soka Tanzania Bara
Wajumbe Wa Kamati Ya Utendaji TFF Wampongeza Rais Malinzi