Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, January Makamba amesema kuwa Serikali itaendelea kutafuta fedha kwa wafadhili na wadau wa maendeleo ili kupambana na changamoto ya mabadiliko ya tabianchi.

Ameyasema hayo mara baada ya kufanya ziara ya kukagua ujenzi wa ukuta wa kuhimili wingi wa maji na upandaji wa mikoko katika eneo la Kilimani na Kisakasaka mjini Unguja.

“Athari za mabadiliko ya tabianchi ni dhahiri kwa sasa, sisi kama serikali tunachukua hatua za dhati ikiwa ni pamoja na kutafuta fedha  sehemu mbalimbali duniani ili kuendelea kutekeleza miradi mingi zaidi kama hii ya kupanda mikoko na kujenga kuta zitakazosaidia kupunguza kasi ya maji kufika kwenye makazi ya watu,”amesema  Makamba.

Aidha, Makamba ameainisha kuwa lengo la Serikali ni kulinda na kuokoa uchumi wa wananchi wa kuweka miundombinu wezeshi kwa ustawi wa maendeleo endelevu.

Kwa upande wake, msimamizi wa mradi huo Mhandisi, Khamis Nassoro amesema kuwa changamoto kubwa ni uelewa mdogo wa wananchi juu ya hifadhi ya mazingira na kuwataka wananchi wote kufahamu kuwa suala la kutunza na kuhifadhi mazingira si jukumu la serikali bali ni wajibu wa kila mmoja wetu.

Hata hivyo, mradi huo unatekelezwa na Ofisi ya Makamu wa Rais kwa Ufadhili wa Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia mazingira unatarajiwa kukamilika ndani ya miezi minne na utagharimu dola za kimarekani 74,166.02.

Uteuzi wa Mugabe kuwa balozi wa 'WHO' waibua maswali
Serikali ya Hispania kutangaza hatua dhidi ya jimbo la Catalonia