Waziri wa nchi, Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, kapteni mstaafu George Mkuchika, amesema Serikali ipo mbioni kuajiri zaidi ya watumishi 49,356 katika mwaka ujao wa fedha utakaoanza Julai mwaka huu.

Amezungumza hayo bungeni pindi alipokuwa anahitimisha hoja ya makadirio ya bajeti ya wizara yake ya mwaka wa fedha 2018/2019.

Ambapo ametaja maeneo mbalimbali yatakayotoa ajira hizo ikiwa ni pamoja na walimu wa shule za msingi na sekondari kwa nafasi 16,000, kada ya afya nafasi 15,000 na nafasi zilizobaki ni kwaajili ya kada nyinginezo kama vile mifugo, kilimo, uvuvi, vyombo vya usafiri, magereza, uhamiaji, watendaji na wahadhiri.

Ameongezea kuwa Serikali katika mwaka huu wa fedha wametenga nafasi 162,221 kupandisha vyeo watumishi wenye sifa stahiki wa kada mbalimbali.

Pia ameeleza kuwa katika nafasi hizo, nafasi 2044 zimetengwa kwa ajili ya kuziba mapengo mbalimbali.

”Uteuzi huu utapunguza nafasi za kukaimu. Natoa rai kwa mamlaka nyingine zinazohusika kuhakikisha kuwa zinaanzisha mchakato mapema kwa kuzingatia vigezo vya miongozo mbalimbali, kuhusu nyongeza za mishahara kama lilivyojadiliwa na wabunge wengi, Serikali inakusudia kutoa nyongeza ya mwaka kwa mujibu wa kanuni za utumishi wa umma” Amesema Mkuchika.

Hata hivyo Mkuchika amefafanua kuwa Serikali ilisimamisha zoezi la kuajiri kupisha zoezi la kuhakiki vyeti vya taaluma vya watumishi wa umma, hata hivyo uhakiki huo umekwishakamilika, na tayari Serikali imeajiri watumishi mbadala kuziba nafasi za watumishi walioumbuliwa kwa kumiliki vyeti feki na zoezi la kuajiri watumushi wapya bado linaendelea.

Diamond ajitoa mkavu, ‘kama sio mimi wa jana vile..’
Umoja wa Ulaya wagawanyika, wahofia maamuzi yatakayochukuliwa na Urusi