Serikali imesema kuwa Ofisi ya Taifa ya Takwimu inawajibu wa kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa kuandaa, kusambaza na kutumia takwimu rasmi na bora ili kuweza kukabiliana na changamoto za kitakwimu walizonazo.

Hayo yamesemwa jijini Dodoma na Naibu Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Ashatu Kijaji ,wakati wa maazimisho ya siku ya Takwimu Afrika ambapo amesema kuna madhaifu makubwa katika halmashauri ambayo yanapelekea kutekeleza programu na miradi mingi ya maendeleo kwa kiwango cha chini.

Amesema kuwa Serikali haiwezi kuboresha huduma za jamii kama jamii husika haijui umuhimu wa takwimu katika kupanga, kutekeleza, kufuatilia na kusimamia programu na miradi mbalimbali ya maendeleo katika maeneo yao.

Dkt.Kijaji amesema kuwa kuna changamoto nyingi za upotoshaji unaofanywa na watu na taasisi mbalimbali hapa nchini, na kusema kuwa sheria ya takwimu ya mwaka 2015 na kanuni zake imebainisha utaratibu wa kuandaa na kusambaza takwimu rasmi na bora.

“Ni jukumu la Ofisi ya Taifa ya Takwimu kutoa elimu kwa umma kuhusu athari na madhara ya kupotosha takwimu, mbalimbali na kutoa elimu pia mnapaswa kukemea na kuchukua hatua dhidi ya wale wote wanao potosha umma kwa makusudi au kwa kutumiwa na taasisi au watu wenye maslahi binafsi”amesema Ashatu.

Dkt.Kijaji amesema kuwa kifungu cha 24B (1) kinakataza mtu kutoa taarifa za kitakwimu zenye lengo la kupotosha umma pamoja na adhabu inayostahili kutolewa kwa yeyote atakaye fanya hivyo,mmepewa mamlaka haya kisheria hivyo simamieni sheria kwa maslahi mapana ya taifa letu na si vinginevyo.

Aidha amesema kuwa changamoto nyingine ni kukosekana kwa kada ya takwimu katika muundo wa serikali na taasisi zake kwani hakuna idara wala Ikama ya kada ya takwimu katika Wizara,Idara zinazojitegemea, Wakala, Mashirika na Mamlaka za serikali za mitaa.

Naye Mtakwimu Mkuu wa Serikali Ofisi ya Taifa ya Takwimu Albina Chuwa amesema kuwa lengo kuu la kuasisi maadhimisho hayo ni kuelimisha umma katika bara la Afrika kuhusu umuhimu wa takwimu na kuongeza ufahamu kuhusu nafasi na mchango wa tasnia ya takwimu katika kuleta maendeleo ya kiuchumi na kijamii barani aAfrika.

 

Didier Drogba awaachia vijana
JPM afanya uteuzi mwingine