Serikali imesema kuwa itaanza kujenga daraja la Mto Momba litakaloiunganisha Mikoa ya Rukwa na Songwe kwaajili ya kuondoa kero kwa wananchi ambayo imekuwa ikiwasumbua hasa wakati wa masika.

Hayo yamesemwa Naibu waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano, Eng. Edwin Ngonyani mara baada ya ziara ya ukaguzi wa barabara Kasansa mpaka Kilyamatundu ambapo amesema kuwa tayari Serikali imeshampata mkandarasi atakayejenga daraja hilo.

“Serikali imeshatoa kiasi cha sh. Bilioni tatu  fedha hizo zimetusaidia kutangaza zabuni na kumpata mkandarasi, tayari Mkandarasi wa ujenzi huu ameshapatikana na mkataba wa makubaliano ya ujenzi umeshakamilika hivyo mkandarasi atausaini rasmi hivi karibuni,” amesema Eng. Ngonyani.

Aidha, Eng.Ngonyani amesema kuwa ujenzi na kukamilika kwa daraja hilo kutasaidia kukuza uchumi na wa wananchi wa mikoa hiyo, hivyo kuongeza pato la taifa wakati huu nchi inaelekea kwenye uchumi wa kati wa Viwanda

Vile Vile amemuagiza Meneja Wa Wakala wa barabara (TANROADS) Mkoa wa Rukwa kuhakikisha anatoa ajira kwa wakazi waliopo kata ya Kipeta ambapo ujenzi wa daraja hilo utafanyika.

Hata hivyo, kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Kwela, Ignas Malocha ameishukuru Serikali ya awamu ya tano ya Dkt. John Magufuli kwa kutekeleza ahadi ya ujenzi wa daraja hilo ambalo kukamilika kwake kutawaletea maendeleo wakazi hao kwa vile litaufungua Mkoa wa Rukwa na kuunganisha na Songwe na Katavi.

Naye meneja wa TANROADS Rukwa Eng. Msuka Mkina amewahakikishia wakazi kijiji cha  Kilyamatundu kuwa Wakala utasimamia ujenzi huo ili ukamilike kwa wakati na viwango na kupitia mradi huo wananchi hao watapata ajira.

 

Los Angeles Galaxy Yamtengea Pauni Milion 6 Kwa Mwaka
Abdelhak Nouri Huenda Asicheze Tena Soka