Serikali ya jiji la Dubai katika Umoja wa Falme za Kiarabu umekana madai ya Mfalme wa RnB, R Kelly kuwa ana matamasha kadhaa ya kufanya jijini humo.

Ijumaa iliyopita, R Kelly aliiomba mahakama kumpa nafasi ya kuweza kusafiri hadi Dubai kwa lengo la kufanya matamasha kadhaa, ingawa anaendelea na mchakato wa kesi ya unyanyasaji wa kingono wa wasichana wadogo inayomkabili.

Hata hivyo, mtandao wa TMZ umewasiliana na Ofisi ya Vyombo vya Habari ya Dubai (Dubai Media Office) kuhusu suala hilo, na imesema hakuna biashara yoyote ambayo jina la R Kelly limetajwa hivi karibuni.

“Serikali hapa Dubai haijapokea maombi yoyote ya kufanyika tamasha ambalo R Kelly atatumbuiza na hakuna ukumbi wowote ambao umechukuliwa kwa ajili hiyo,” Dubai Media Office imeeleza kwenye taarifa yao.

Hata hivyo, ombi la R Kelly kwa mahakama lilikumbana na changamoto kutokana na uzito wa mashtaka yanayomkabili.

R Kelly alianza kujitetea mahakamani wiki iliyopita akikana video zilizowasilishwa kama ushahidi kuwa anawanyanyasa kingono wasichana wadogo.

Mwimbaji huyo yuko nje kwa dhamana akikabiliwa na kesi mahakamani lakini pia pigo la kukataliwa na kutengwa na wasanii wenzake ambao walitumia makala ya ‘Surviving R Kelly’ kuchukua uamuzi wa kuondoa mtandaoni nyimbo walizomshirikisha.

JPM atoa zawadi ya viwanja kwa wachezaji wa Taifa Stars
Live Ikulu: Rais Magufuli akizungumza na wachezaji Taifa Stars, bondia Mwakinyo