Kiongozi wa Muungano wa Upinzani nchini Kenya Nasa, Raila Odinga amefunguka kuhusu mazungumzo aliyoyafanya na Rais Uhuru Kenyatta walipokutana mapema mwezi huu.

Amesema kuwa wamefanya mazungumzo na kufikia baadhi ya makubaliano kuhusu mauaji yaliyotokea kipindi cha uchaguzi na sakata la kujiapisha kwa Raila Odinga.

Amesema wamekubaliana kwamba waathirika wote kupitia ghasia za uchaguzi wa mwaka 2017 watalipwa fidia na serikali.

”Watu wengi waliuawa kufuatia uchaguzi wa mwaka jana. Tumekubaliana na Rais Kenyatta matukio yote yaliotendeka kinyume na haki lazima yapatiwe fidia kwa familia zilizoathirika” amesema Odinga.

Lakini pia wameafikiana kufuta kesi za watu walioshiriki katika siku ya kujiapisha kwa Raila Odinga, tukio lililofanyika January 30 mwaka huu.

Kufuatia makubaliano hayo wamelenga kuzika tofauti zao kisiasa kwa maslahi ya taifa la Kenya.

Aidha Odinga amesema kuwa makubaliano hayo yamefanywa kati yao wawili na si kati ya chama cha Nasa na Jubilee.

Rais Uhuru Kenyatta pamoja na Odinga walikutana Ikulu Machi 9 ambapo baada ya mazungumzo yao wote walisema kuwa wamekubaliana kuiunganisha Kenya kwani nchi hiyo ni kubwa kuliko wao.

 

Ulega azitaka halmashauri kutumia fursa
Video: Zitto aanika bajeti mbadala ya wananchi, Mkapa ataka mdahalo wa kunusuru elimu