Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Faustine Ndugulile amelaani mauaji na matendo ya kikatili yote yanayofanywa dhidi ya Watoto, huku akivishukuru vyombo vya Dola kwa hatua za haraka wanazoendelea kuchukua katika kudhibiti matukio hayo.

Ameyasema hayo jijini Dar es salaam wakati alipofanya ziara ya kukagua hali ya Makazi ya Watoto wanaoishi katika Mazingira magumu yaliyopo Kurasini,

Amesema kuwa Serikali haiwezi kuvumilia mambo yakikatili yanayofanywa dhidi ya Watoto na haki zao, hivyo itawachukulia hatua yeyote atakaye bainika amekwenda kinyume na kuvunja sheria zinazomlinda mtoto.

“Tunalaani sana, mauaji haya ya Watoto, na tunavishukuru vyombo vya Dola vimeweza kuchukua hatua za haraka kuhakikisha kwamba vinadhibiti matukio haya,” amesema Dkt. Ndugulile

Aidha, Dkt. Ndugulile ametoa rai kwa Waganga wote wa Tiba Asili na Tiba Mbadala kuacha kutumia viungo wala miili ya Watoto kama njia yakutatua matatizo kwa wateja wao, hivyo hatua kali zitachukuliwa kwa watakao kaidi agizo hilo.

Dkt. Ndugulile pia ameutaka Uongozi wa Makazi ya watoto waishio katika mazingira magumu kuwajibika katika baadhi ya mambo ikiwemo masuala ya usafi wa mazingira, Mabweni na mavazi kwa watoto uzingatiwe na kuaagiza kuweka magodoro mapya, mashuka na chandarua  katika mabweni hayo.

Kwa upande wake Afisa Mfawidhi wa Makazi hayo, Beatrice Mgumiro amesema kuwa makazi hayo yana jumla ya watoto 70 ambapo watoto 54 wapo katika makazi hayo na watoto 16 wapo wanasoma katika shule za Bweni.

 

RC Ole Sendeka atajwa mkoani Njombe
Kangi Lugola amng'oa mkuu wa kituo cha Polisi Mang'ola