Naibu Waziri wa Afya dkt. Faustine Ndugulile, amesema Serikali imetuma wataalamu wake kwaajili ya kumhoji Nabii Moses Mollel maarufu kama namba saba aliyejitokeza na kutangaza kuwa anao uwezo wa kutibu ugonjwa wa homa kali ya mafua inayosababishwa na Virusi vya Corona na iliyopewa jina la COVID-19.

Dkt Ndugulile amesema kuwa endapo watabaini mtu huyo hana utaalamu katika kile alichokitangaza, Serikali itamchukulia hatua stahiki na kuwataka wananchi kuepuka kutoa kauli ambazo zitachanganya jamii.

“Sisi tumeona hizo clip ambazo zinazunguka na sisi tumetuma timu yetu ya wataalamu ili huyo bwana akatuthibitishie kama ana uwezo wa kufanya tiba hiyo na atuambie hiyo dawa yake imesajiliwa wapi na yeye amesajiliwa wapi na lini” amesema Dkt Ndugulile.

Hayo yamejiri baada ya hivi karibuni kusambaa video mbalimbali katika mitandao ya kijamii, zikimuonesha Mosses Mollel, maarufu kama Nabii namba saba, kwamba anao uwezo wa kutibu virusi vya Corona.

Moses, mkazi wa Ngaramtoni mkoani Arusha amekuwa akijitangaza kuwa na dawa ya kutibu ugonjwa huo na kuweka mawasiliano yake kwenye mitandao.

Australia: Maafisa wafanikiwa kuzima moto wa muda mrefu
Kaya masikini zaidi ya milioni moja kusaidiwa na Tasaf