Serikali kupitia Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu ametangaza ongezeko la  masaa ya unyonyeshaji kwa watoto kwa watumishi wa serikali, mashirika pamoja na sekta binafsi ili kuwezesha watoto kuwa na afya bora inayotokana na maziwa ya mama.

Ummy Mwalimu amezungumza hayo wakati akifungua Wiki ya Unyonyeshaji, amesema kuwa mama mzazi baada ya kumaliza miezi mitatu ataingia kazini saa 3:30  asubuhi na kuondoka saa 7:30 Mchana katika kumuwezesha mama kunyonyesha mtoto bila kuingiliwa na majukumu ya kikazi.

Ummy amesema kuwa watendaji wa Umma na mashirika pamoja na taasisi binafsi lazima wafanye hivyo katika kutambua umuhimu wa mama mzazi kunyosha kwa muda uliowekwa kwa kipindi cha miezi sita.

Waziri Ummy amesema kuwa ni gharama kubwa katika kuhudumia watoto walio na utapiamlo ambao unatokana na mtoto kukosa maziwa ya mama kwa muda mrefu hivyo kuepuka jambo hilo njia rahisi ikiwemo kutengwa kwa masaa hayo. Pia Waziri amedai suala la lishe lazima liangaliwe kwa ukaribu na wadau wote katika kuweza kuwaondoa watoto katika utapiamlo ambao unafanya kudumaa kwa akili.

Nae Mkurugenzi Mtendaji wa Chakula na Lishe Nchini(TFNC), Joyceline Kaganda amesema jitihada mbalimbali zimekuwa zikifanyika juu ya masuala ya lishe na wadau kwa mifumo mbalimbali. Amesema wiki ya unyonyeshaji wa kina mama ni muhimu katika ukuaji wa mtoto kwa kumjenga katika afya bora.

Video: Goodluck Gozbert atoa mpya nguvu ya 'shukrani'
Rais Magufuli awapandisha vyeo na kuwateua maafisa wawili wa zimamoto