Wananchi kutoka vijiji vitano Kata ya Mdandu Wilayani Wanging’ombe, Njombe kwa kushirikiana na Mbunge wa jimbo hilo, Gerson Lwenge wameshiriki kuandaa eneo kwa ajili ya ujenzi wa hospital ya wilaya ekari 80 katika Kijiji cha Ihanja baada ya Serikali kuleta fedha shilingi milioni 500 kati ya bilioni moja inayohitajika.
Akizungumza  na wananchi katika eneo ambalo kutajengwa hospital hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa halmashauri  ya wilaya ya Wanging’ombe, Edes Lukoa amesema kwa awamu ya kwanza tayari Serikali imeleta milioni 500.
‘’Serikali kuu kwa awamu ya kwanza imeleta shilingi milioni 500, naipongeza Serikali ya awamu ya tano kwamba maneno kidogo vitendo zaidi…kwa hiyo hizo zimefika na bajeti ni bilioni 1 na milioni 500 na natumai ifikapo tarehe 30 juni mwakani fedha zote zitakua zimefika’’amesema Lukoa.
“Huu mradi ni wa kwenu nyinyi wananchi ni vizuri zaidi mshiriki kila hatua…kuanzia upande wa mafundi hadi kazi nyingine ili tuweze kukalimisha kwa wakati” ameongeza Lukoa.
Kwa upande wa mbunge wa jimbo hilo amesema Serikali itaendelea kuleta fedha kadri ujenzi unapokuwa ukiendelea.
‘’Safari tuliyonayo ni ndefu, fedha hizi hazijaja kama mvua na mkiona vyaelea ujue vimeundwa….msilete siasa katika masuala ya maendeleo na hivyo tushiriki kikamilifu ili kuweza kukamilisha jambo hili “amesema Lwenge.
Aidha, mkazi wa kijiji cha Ihanja, Alex Mtamba amesema wamejitokeza ili kuandaa eneo  ili kutatua changamoto ya upatikanaji wa huduma ya afya ambapo awali walikuwa wakifuta huduma hiyo katika hospital ya kibena mjini Njombe.
‘’Hili eneo la ekari 80 tumelitoa sisi wenyewe na kuhakikisha linakua tayari kwa ujenzi tunashukuru serikali kwa kuleta fedha hizi na endapo ujenzi utaanza na kukamilika changamoto za huduma za afya zitaisha…zamani wanawake walikuwa wanatembea umbali mrefu kwenda Njombe mjini ambapo ata wengine walipoteza maisha’’ amesema Mtamba.

Mahakama yawaachia huru Diane Rwigara na mama yake
Benki ya TPB yaandaa mkutano wa mabenki ya Akiba Afrika Mashariki