Serikali imetoa shilingi bilioni 24.496 kwa ajili ya kujenga meli mpya mbili na kukarabati meli tano ili ziweze kutoa huduma ya uchukuzi wa kusafirisha abiria na mizigo katika maziwa makuu ya Victoria, Tanganyika na Nyasa.

Hayo yamesemwa hii leo Bungeni Mjini Dodoma na Naibu Waziri wa Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Mhandisi, Atashasta Nditiye alipokuwa akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa Kampuni ya Huduma za Meli (MSCL) kwa wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge na Miundombinu kuhusu ujenzi wa meli katika maziwa makuu.

Amesema kuwa fedha hizo tayari zimeshatolewa na Serikali na kupatiwa Kampuni ya MSCL kwa ajili ya kuanza ujenzi wa meli 2 mpya za kubeba abiria na mizigo katika ziwa Tanganyika na Victoria na kukarabati meli 5 ambazo ni MV. Victoria, MV. Butiama, MV. Liemba, MV. Umoja na MV. Serengeti.

Aidha, amesema kuwa lengo la Serikali la kutoa fedha hizo ni kuboresha huduma za usafirishaji wa abiria na mizigo katika maziwa makuu ili wananchi waweze kupata huduma za usafiri wa uhakika.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Miundombinu Prof. Norman Sigalla ameipongeza Serikali kwa kutoa fedha za kujenga na kukarabati meli za maziwa makuu.

 

Aliyewadunga wanawake ‘mimba feki’ atiwa mbaroni
Matumizi ya jezi ya Mafisango yalivyowakera wadau